F Daraja la Tipri Mbulu: Mkombozi wa Mawasiliano kwa Wananchi | Muungwana BLOG

Daraja la Tipri Mbulu: Mkombozi wa Mawasiliano kwa Wananchi


Na John Walter-Manyara

Daraja la wapita kwa miguu la Tipri katika Wilaya ya Mbulu, mkoani Manyara, limeendelea kuwa mkombozi mkubwa kwa wananchi wa eneo hilo baada ya kumaliza changamoto ya mawasiliano iliyodumu kwa muda mrefu.

Kabla ya ujenzi wa daraja hilo la kamba lililosimamiwa na Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA), wananchi walikosa njia salama ya kuvuka kutoka eneo moja kwenda jingine, hali iliyosababisha huduma muhimu kama elimu, afya na biashara kukwama.

Wanafunzi wa Shule ya Msingi Tipri wanasema daraja hilo limewarahisishia kufika shuleni kwa wakati na kwa usalama zaidi. 

Mwalimu wa shule hiyo, Josephine Dangati, anabainisha kuwa daraja hilo limepunguza utoro na kuchelewa kwa wanafunzi, jambo linalochangia kuboresha ufaulu wa kitaaluma.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa kitongoji cha Tsawa, kijiji cha Tsawa, Isaack Gwandu, amesema ujenzi wa daraja hilo limeongeza furaha kwa kijamii na kuchochea shughuli za kiuchumi kwa kuwa wananchi sasa wanavuka kwa urahisi kusafirisha bidhaa na kupata huduma mbalimbali.

Akizungumzia mradi huo, Meneja wa TARURA Wilaya ya Mbulu, Mhandisi Nuru Hondo, amesema daraja hilo ni sehemu ya juhudi za serikali kuboresha miundombinu ya usafiri vijijini ili kurahisisha maisha ya wananchi likijengwa Kwa shilingi Milioni 147.

Naye Meneja wa TARURA Mkoa wa Manyara, Mhandisi Salim Bwaya, amesisitiza kuwa TARURA itaendelea kujenga na kuboresha madaraja na barabara ili kuhakikisha mawasiliano yanakuwa ya uhakika mwaka mzima.

Kwa sasa, wananchi wa Tipri wanaeleza furaha yao huku wakilitaja daraja hilo kama alama ya maendeleo na matumaini mapya kwa jamii yao.

 

Chapisha Maoni

0 Maoni