F Rabia na Sendiga Wasisitiza Bima ya Afya kwa Wote Manyara | Muungwana BLOG

Rabia na Sendiga Wasisitiza Bima ya Afya kwa Wote Manyara


Na John Walter-Manyara

Katibu wa NEC Siasa na Uhusiano wa Kimataifa wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndugu Rabia Abdallah Hamid, kwa pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga, wamewahimiza wananchi kujiunga na mpango wa Bima ya Afya kwa Wote ili kuhakikisha upatikanaji wa huduma za afya kwa uhakika.

Wameyasema hayo wakati wakizungumza na mamia ya wananchi wa Kata ya Gidahababieg, Wilaya ya Hanang, katika maadhimisho ya kuzaliwa kwa Chama Cha Mapinduzi yaliyofanyika mkoani Manyara.

Akizungumza katika mkutano huo, Ndugu Rabia Abdallah Hamid amesema dhamira ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ni kuhakikisha kila Mtanzania anakuwa na uhakika wa kupata matibabu pindi anapokumbwa na dharura za kiafya kupitia mpango wa Bima ya Afya kwa Wote.

Ameeleza kuwa ugonjwa haubishi hodi, hivyo kuwa na bima ya afya ni kinga muhimu kwa wananchi kwani huwapa uhakika wa matibabu wakati wowote bila changamoto za kifedha.

Aidha amewahimiza wananchi kumuunga mkono Rais Dkt. Samia katika utekelezaji wa mpango huo ili kuimarisha ustawi wa afya zao.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga, amesema utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM katika mkoa wa Manyara unaendelea kwa kishindo kwa asilimia 100.

Ametolea mfano utekelezaji wa ahadi za Rais Dkt. Samia katika siku 100 za awali za uongozi wake, hususan katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za afya kupitia kuanzishwa kwa mpango wa Bima ya Afya kwa Wote.

Mhe. Sendiga amesema kuwa mpango huo tayari umeanza kutekelezwa mkoani Manyara, ambapo wananchi wanaendelea kupewa elimu kuhusu umuhimu wa bima ya afya, huku wanufaika wa makundi maalum tayari wakishapatiwa kadi zao za bima.

Viongozi hao wameeleza kuwa mpango wa Bima ya Afya kwa Wote ni mkombozi mkubwa kwa wananchi, hasa ikizingatiwa kuwa baadhi ya watu wamekuwa wakishindwa kupata matibabu au hata kuchukua miili ya wapendwa wao hospitalini kutokana na kukosa fedha.

Maadhimisho hayo yalifanyika chini ya kauli mbiu isemayo “Tumechagua Umoja na Amani kwa Maendeleo ya Taifa Letu.”

 


Chapisha Maoni

0 Maoni