Na John Walter-Babati
Mkutano wa hadhara wa kusoma mapato na matumizi ya Kijiji
cha Magugu umebaini upungufu wa madawati 432 katika shule tano za kijiji hicho,
hali inayohitaji zaidi ya shilingi milioni 34 ili kuziba pengo hilo.
Mkutano huo ulioongozwa na Mwenyekiti wa Kijiji, Loya
Amos, uliwakutanisha wananchi na viongozi wa kijiji kujadili hali ya
maendeleo pamoja na vipaumbele vinavyohitaji utekelezaji wa haraka.
Wakichangia hoja katika mkutano huo, wananchi wamesema
maendeleo ni yao na wako tayari kushiriki kikamilifu endapo watawekewa
utaratibu rafiki na wazi utakaowezesha kuwashawishi kuchangia miradi ya
maendeleo.
Kwa upande wake, uongozi wa kijiji kupitia mwenyekiti na
kamati ya maendeleo uliwahakikishia wananchi kuwa utazungumza kwanza na wadau
wa maendeleo ili kutafuta msaada, na kiasi kitakachobaki ndipo wananchi
watashirikishwa kuchangia.
Hatua hiyo ilipokelewa na kuungwa mkono na wanakijiji
waliohudhuria mkutano huo.
Viongozi wa kijiji wamesisitiza umuhimu wa ushirikiano kati
ya wananchi na uongozi katika kutatua changamoto za elimu, wakieleza kuwa
upatikanaji wa madawati ya kutosha utaboresha mazingira ya kujifunzia kwa
wanafunzi.

0 Maoni