inaweza kuwa ndiyo siku muhimu kuliko zote mwaka huu kwa
Watanzania. Hiyo inatokana na ukweli kwamba ni siku ambayo wananchi 22.75
milioni wanatarajiwa kupiga kura kuchagua viongozi watakaoiongoza nchi yetu kwa
miaka mitano ijayo. Si ajabu kwamba kila Mtanzania anajua umuhimu wa Oktoba 25
ingawa wapo wanaojua zaidi. Wachambuzi wa mambo wanabashiri uwezekano wa
kubadilisha historia ya nchi ya Tanzania
kwa kupata kiongozi kutoka chama mbadala, mbali na CCM kinachotawala sasa.
Hata hivyo, zipo kumbukumbu zinazoonyesha mustakabali wa
baadhi ya nchi ulibadilika baada ya uchaguzi mkuu wa kidemokrasia.
Wapo viongozi mashuhuri duniani wanaoendelea kukumbukwa
kutokana na matukio ya vurugu waliyofanya baada ya uchaguzi kwenye mataifa yao .
Hata hivyo, dalili
zinaonyesha uchaguzi wa mwaka huu utakaokuwa wa 14 tangu kuanza kutumika kwa
mfumo wa vyama vingi kabla na baada ya uhuru utakuwa na ushindani mkubwa.
Historia ya uchaguzi
Kumbukumbu zinaonyesha uchaguzi wa vyama vingi umewahi
kufanywa mara tatu katika awamu tofauti enzi za Tanganyika, mbili kati ya hizo zikifanyika kabla ya uhuru,
yaani mwaka 1958 na 1960 na wa tatu
ulifanyika Novemba Mosi mwaka 1962, baada ya uhuru na kabla ya Muungano wa Tanganyika na
Zanzibar mwaka 1964.
Baada ya hapo ilipita miongo mitatu ya utawala wa chama
kimoja iliyoshuhudia chaguzi sita; mwaka 1965, 1970, 1975, 1980, 1985 na ule wa
1990.
Mfumo wa vyama vingi ulirejeshwa mwaka 1992 na kwa kipindi
hicho chote, uchaguzi mkuu umefanyika mara nne zilizoendeshwa kwa utulivu na
amani; mihula miwili ya awamu ya tatu ya Rais Benjamin William Mkapa (1995-
2005) na miwili mingine ya Rais Jakaya Mrisho Kikwete (2005-2015) ikiwa awamu
ya nne.
Nguvu ya NEC
Historia hiyo ya mafanikio kwenye uchaguzi, inaipa nguvu
Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kuamini hata mwaka huu hakuna litakalo
haribika, bali historia itaendelea kutunzwa ili ulimwengu uendelee kujifunza
kutoka Tanzania .
Mwenyekiti wa tume
hiyo, Jaji Mstaafu, Damian Lubuva analithibitisha hilo kwa wadau wote waliokutana na taasisi
hiyo nyeti katika maandalizi ya siku uchaguzi mkuu inayosubiriwa na Watanzania
22, 782, 558 wanaotarajiwa kupiga kura.
Ili kuwaandaa wapiga kura kutekeleza haki yao ya kikatiba kwa amani na utulivu kwa wiki
mbili mfululizo, NEC imefanya mazungumzo na makundi yote yanayowakilisha jamii.
Ilianza na viongozi wa dini; maaskofu na masheikh wakafuata wawakilishi wa
walemavu kisha Wamiliki wa Vyombo vya Habari (MOAT).
Wahariri wa vyombo vyote vya habari nchini chini ya jukwaa
lao (TEF), pia vijana na wanawake, mmoja kutoka kila mkoa wakiwakilisha asasi
zinazohusika na makundi hayo ili wafikishe elimu stahiki kupitia taasisi zao.
Kundi la mwisho lilikuwa viongozi wote wa vyama vya siasa 22
vinavyoshiriki uchaguzi mkuu wa mwaka huu. Ni kundi muhimu zaidi ambalo kero
zake ni lazima zisikilizwe na kutatuliwa kwa wakati kwani ndilo linaloweza
kuamua uchaguzi huu uweje; wa amani au vurugu.
NEC pia ilikutana na wataalamu wa Tehama wa vyama vya siasa
na waangalizi wa kimataifa, waliotanguliwa na kundi la waratibu (30) na
wasimamizi (972) wa uchaguzi kutoka halmashauri zote nchini na makamanda wa polisi kutoka mikoa na
kanda maalumu zilizopo nchini.
NEC inawaagiza wajumbe wa mkutano huo kutenda haki kwenye
uchaguzi mkuu wa mwaka huu ikikumbusha dhamana ya usalama wa taifa iliyo
mikononi mwao na kutahadharisha kwamba kosa lolote linaweza kuliingiza taifa
kwenye matatizo na kumtaka kila mmoja kutimiza wajibu wake ipasavyo.
Jaji Lubuva anatoa rai hiyo huku akielezea falsafa ya
uchaguzi ya Jonas Savimbi, aliyekuwa kiongozi wa vita vya msituni wa nchini Angola ambaye
alifariki Februari 22, 2002.
Anasema: “Mwandishi mmoja wa vitabu anaielezea vizuri
falsafa ya uchaguzi ya Savimbi; kiongozi huyo aliamini kuwa yeyote anayeshiriki
uchaguzi ni lazima ashinde na asiposhinda basi ameibiwa kura. Hivyo hatakiwi
kukubali matokeo, badala yake anatakiwa apambane kuhakikisha anashinda.”
Kwa miaka 27, Jonas Malheiro Savimbi aliendesha mapambano ya
msituni dhidi ya Serikali ya Angola .
Alianza kwa kujiunga na chama cha wapigania uhuru wa MPLA mwaka 1964, muda
mfupi baadaye akajiunga na chama cha FNLA. Miaka miwili baadaye, 1966,
alianzisha vuguvugu la Unita zikiwa harakati ya kuikomboa Angola kutoka
ukoloni wa Ureno.
Lubuva anasema hakuna anayetarajia kuona falsafa ya Savimbi
inatumika nchini baada ya Oktoba 25 kwani wadau wote walioshirikishwa wametoa
uzoefu wao na kubainisha changamoto zinazohitaji kufanyiwa kazi kwa wakati
kabla ya upigaji kura.
Pia wenye majukumu wameelezwa cha kufanya; kabla, wakati na
baada ya mchakato huo. Kwa maandalizi hayo, kila mdau anatarajiwa kutosheka na
kilichofanywa.
Waratibu, wasimamizi
na polisi
Licha ya kuwakutanisha pamoja na kubadilishana uzoefu, NEC
ilikabidhi mamlaka ya kutenda haki kwa wagombea ubunge na udiwani kwa
Wakurugenzi wa Halmashuri husika chini ya uangalizi wa Jeshi la Polisi
ikiwataka watumie weledi kuwahudumia wateja wao baada ya upigaji kura
kufanyika.
Mwenyekiti wa NEC anawaasa watendaji hao kushirikiana kwa
kila changamoto itakayojitokeza na kuitatua bila kusababisha madhara kwa jamii
inayowazunguka na wafanye hivyo bila upendeleo.
“Hii ni mara ya kwanza kwa NEC kuwakutanisha watendaji na
makamanda wa polisi kabla ya uchaguzi mkuu. Awali tulikuwa tunakutana na kila
kundi kwa wakati wake. Leo tutapeana taratibu zote muhimu za uchaguzi kuanzia
upigaji, kuhesabu, ujumlishaji wa kura mpaka utangazaji wa matokeo. Tutumie
mkutano huu kujifunza makosa yote yaliyotokea kwenye chaguzi zilizopita.
Kumbukeni, kosa moja dogo linaweza kuleta uvunjifu wa amani
kwenye maeneo yenu na hata kuliingiza taifa kwenye matatizo. Hivyo, fanyeni
kazi kwa weledi, uadilifu na fuateni sheria, kanuni na taratibu za NEC,”
anasema Jaji Lubuva.
Kiongozi huyo pia anabainisha mkakati wa tume yake kuufanya
uchaguzi kuwa wa haki, huru na kuaminika zaidi akimtaka kila mmoja kuzingatia maelekezo na
makubaliano, wakiwamo mawakala wa vyama vya siasa.
“Uzoefu wa chaguzi
zilizopita na taarifa tulizonazo, kuna vikundi vya vijana wanaohusishwa na
vyama vya siasa wanaowatisha wapigakura, hasa kina mama ili wasishiriki
mchakato huu. Ni rai yangu mhakikishe hilo
halijitokezi na Watanzania wote watapata haki yao ya kikatiba. Baada ya kupiga kura, endapo
kutakuwa na ulazima watu wasimame zaidi ya mita 200 kutoka kituoni, vinginevyo
warudi makwao wakasubiri kutangazwa kwa matokeo,” anahimiza Lubuva.
Kukiwa na wajumbe wote saba wa NEC, Mkuu wa Jeshi la Polisi
(IGP), Ernest Mangu pamoja na Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai,
Diwani Athumani, Mkuu wa Oparesheni wa Polisi, Paul Chagonja, Mkuu wa Polisi
Jamii, Mussa Alli Mussa na Kamishna wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman
Kova na baadhi ya wakuu wa vikosi, watendaji hao waliaswa kuchukua tahadhari na
kuepusha aina yoyote ya uvunjifu wa amani unaoweza kusababishwa na maamuzi yao.
Kwa upande wake, IGP Mangu anaahidi jeshi lake litatumia
busara kuendeleza utulivu uliopo na kuhitimisha mchakato wa uchaguzi kwa amani,
huku akibainisha changamoto za kiusalama zilizopo mwaka huu.
Anaitaja ya kuwaweka watu umbali wa mita 200 kutoka kilipo
kituo cha kupigia kura, akisema inahitaji busara kwa sababu vingi vipo karibu
na makazi ya watu, hivyo askari wake watalazimika kuwa makini ili kutovunja
haki wakati wakisimamia sheria hiyo.
“Mazingira ya kidemokrasia yamebadilika sana nchini. Ni tofauti na mwaka 2010 au
kabla ya hapo, ndiyo maana hata matumizi ya nguvu yamepungua mwaka huu. Mara
nyingi tunasikilizana na wanasiasa…kwa hali hiyo nguvu haijahitajika katika
mikutano mingi ya kampeni zinazoendelea,” anasema Mangu.
Wanawake
Jaji Lubuva pia anawaambia wawakilishi wa wanawake kuwa NEC
inatambua mchango wa asasi za kiraia zinazowakilisha wanawake katika
kufanikisha uchaguzi nchini.
Anasema anatambua ushawishi, taaluma, vipaji na ujuzi
walionao katika kuelimisha na kuhamasisha wananchi kushiriki katika shughuli
mbalimbali za maendeleo ikiwa ni pamoja na uchaguzi.
“Tutahakikisha mchakato huu unafanyika kwa uwazi, uhuru na
haki zaidi kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa ili kujenga
demokrasia ya kweli na kuimarisha utawala bora,” anasema Lubuva.
Wawakilishi hao wanapewa jukumu la kufikisha elimu kwa jamii
kwamba siku ya uchaguzi, vikongwe, wajawazito na wenye watoto wachanga
hawapaswi kupanga foleni.
Wahariri
Mkurugenzi wa Uchaguzi wa tume hiyo, Kailima Kombwey
anaeleza uhusiano mzuri uliopo kati ya NEC na wahariri wa vyombo vya habari,
pia wadau wote wa habari akiwakumbusha kujiridhisha kwa kupata taarifa sahihi
kabla ya kupeleka habari zao kwa wananchi.
Anasema: “Pamoja na umuhimu huo, mna jukumu kubwa la
kuhakikisha habari mnazozitoa zinalenga kujenga amani ya nchi na kuepuka
kutojiingiza katika ushabiki wa kisiasa kwa kusahau misingi ya uandishi wa
habari.
Nchi nyingi zimeingia katika machafuko, hasa wakati wa uchaguzi
kutokana na ushawishi wa vyombo vya habari, hasa pale kwa makusudi vinapoamua
kuandika habari za uchochezi na ushabiki, badala ya mambo ya msingi ya sera na
ilani za vyama pamoja na masuala ya maendeleo. ”
Wenye Ulemavu
Mbele ya wawakilishi wa watu wenye ulemavu tume inajinasibu
kuhakikisha kila raia mwenye sifa anapiga kura, wakiwamo watu wenye ulemavu.
Jaji Lubuva anasema tume yake inatambua watu hao wanahitaji msaada wawapo
kwenye vituo vya kupigia kura. Anasema
kwa kuzingatia hilo
imetoa maelekezo kwa wasimamizi wa vituo namna ya kuwahudumia.
“Watu wanaoishi na ulemavu watapewa nafasi ya upendeleo
kuingia na kupiga kura pasipo kusimama katika mstari kwa muda mrefu. Kwa
kushauriana na wawakilishi wa walemavu wasioona tumeamua kutumia kifaa maalumu
cha “Tactile Ballot Folder” ili waweze kupiga kura wenyewe bila ya kusaidiwa na
mtu, hivyo kutimiza lengo la usiri wa kura,” anasema.
Vijana
Kutokana na dalili za baadhi ya vyama na wagombea
kuwategemea vijana kufanikisha malengo yao , NEC
inaliasa kundi hilo
kuwa makini na kuhakikisha elimu inafika kwa rafiki zao lakini pia kuepuka
ushabiki.
“Upo mtego wa kuwatumia. Jiangalieni na muwe makini na gilba
za kisiasa. Epukeni kufuata mkumbo…kesho yenu inategemea kwa kiasi kikubwa na
mnachokifanya leo,” anasema Mkurugenzi wa Uchaguzi NEC.
Vyama vya siasa
Makamu Mwenyekiti wa NEC, Jaji Mstaafu Himid Mahmoud Himid
anawaasa viongozi wa vyama vya siasa nchini kujenga uzalendo na kutambua yapo
maisha baada ya uchaguzi, hivyo licha ya kunadi sera wanapaswa kufikiria juu ya
hatima ya wafuasi wa vyama vyao.
