Polisi wakana kumkamata mwandishi wa habari

Jeshi la polisi mkoa wa Njombe limekana kumkamata mwandishi wa habari Emmanuel Kibiki ambaye anadaiwa kukamatwa majira ya saa tisa usiku wa kuamkia leo Februari 22, 2018  na watu waliojitambulisha kuwa ni jeshi la polisi.

Akizungumza na www.eatv.tv Kaimu Kamanda wa polisi mkoa wa Njombe, John Temu amesema kuwa wao hawajamkamata mwandishi huyo na kudai huenda akawa amekamatwa na taasisi zingine ila si jeshi la polisi.

"Hakuna ukweli wowote ule kama kungekuwa na ukweli stori ingekuwa imeshafika kwetu ila inawezekana labda taasisi zingine za upelelezi zinafanya kazi zikawa zimemkamata maana taasisi za upepelezi huwa zinawakamata watu zenyewe, kwa hiyo watu wanapicha tu kuwa mtu akikamatwa basi jeshi la polisi ndilo linakuwa limemkamata.Kwa sababu kama sisi tungekuwa tumemkamata mpaka asubuhi hao polisi wangekuwa wamewasiliana na mkoa kutoa taarifa" alisema John Temu

Februari 22, 2018 zimeibuka taarifa zikidai kuwa mwandishi wa habari wa Makambako amekamatwa majira ya saa tisa usiku na watu ambao walijitambulisha kuwa ni jeshi la polisi lakini upande wa jeshi la polisi wamekataa kuhusika kumkamata mwandishi huyo wa habari.