Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Paul Makonda leo amefungua mkutano mkubwa wa siku tatu wa wataalamu wa masuala ya usafiri kutoka majiji 49 na nchi zaidi ya 30 Duniani waliokuja nchini kujifunza namna Dar es salaam ilivyofanikiwa kwenye usafiri wa mabasi ya mwendokasi na kushika nafasi ya kwanza katika majiji ya Afrika.
Makonda amewaeleza wataalamu hao namna serikali ya awamu ya tano ilivyojidhatiti kuendelea kuboresha sekta ya usafiri ambapo wameshangaa kuona mipango ya serikali kuendelea kujenga miundombinu ya mabasi mwendokasi hadi awamu ya sita.
Aidha Makonda amesema idadi ya wakazi wa jiji la Dar es salaam imekuwa ikiongezeka kila kukicha hivyo uwepo wa miundombinu bora ya usafiri itasaidia kupunguza msongamano wa magari unaopelekea serikali kupoteza mabilioni ya fedha kutokana na foleni.
Mkutano Mkubwa Kama huu kufanyika Dar es salaam ni heshima kubwa kwa Taifa ambapo wataalamu hao watafanya ziara ya kutembelea miundombinu ya usafiri kwa jiji la Dar es salaam kisha kutoa ushauri na mapendekezo kwa mkuu wa mkoa kwaajili ya maboresho.
