Na. Raheli Nyabali, Tabora
Watu wawili wamehukumiwa kifungo cha miaka 40 baada ya kuwakuta na hatia ya kutenda makosa matatu kinyume cha sheria ikiwemo Kesi ya uhujumu uchumi iliyokuwa inawakabili katika mahakama ya hakimu mkazi mkoa wa Tabora.
Akisoma hukumu hiyo hakimu mkazi Mkoa wa Tabora, Jocktan Rushwela amesema mahakama baada ya kupitia maelezo ya mashtaka yaliyowasilishwa na Wakili Upande wa Jamhuri Mercy Ngowi,iliamua kujiridhisha kwa kupitia maelezo ya ushahidi wa pande zote mbili na kubaini kuwa watuhumiwa Ibrahim Mbaruku na Yassin Mohammed walitenda makosa hayo kinyume cha sheria ya uhifadhi na wanyama pori namba tano ya mwaka 2009 wakiwa ndani ya hifadhi ya pori la Ugalla.
Kwa makosa matatu yaliyowatia hatiani katika shitaka hilo la uhujumu uchumi namba 4 la mwaka 2017,kosa la kwanza kuingia ndani ya hifadhi ya msitu wa pori la Ugalla bila kibali halali adhabu iliyotolewa ni kutumikia kifungo cha mwaka mmoja jela au kulipa faini ya shilingi laki moja.
Katika Kosa la pili ambalo ni kukutwa na silaha aina ya Gobore ndani ya hifadhi ya Ugala iliyopo wilayani Kaliua adhabu iliyotolewa ni kutumikia kifungo cha miaka ishirini Jela.
Aidha kosa la tatu ni kukutwa na nyara za Serikali ikiwemo mzoga wa mtoto wa Simba ndani ya Pori hilo la Ugala washtakiwa wamehukumiwa kutumikia kifungo cha miaka ishirini kwa kila mmoja na kufanya jumla ya adhabu ya kifungo cha miaka 41 kwa kila mshtakiwa.
Hakimu mkazi Mkoa wa Tabora, Jocktan Rushwela akafafanua mbele ya washitakiwa hao wawili kwa adhabu ya kosa la pili na la tatu wataitumikia kwa pamoja kwa kifungo cha miaka ishirini huku adhabu ya mwaka mmoja kwa kosa la kwanza ikisalia pale pale.
