Na Adelina kapaya, Katavi.
Mbunge Viti Maalum kupitia Chama Cha Mapinduzi Mkoa wa Katavi Anna Richard Rupembe ametoa mifuko 27 ya Seruji kwa ajili ya ujenzi wa Maabara katika Shule ya Sekondari Kakese pia ametoa bando 5 za bati kwa ajili ya Ujenzi wa nyumba ya Padri katika Kigango cha Mbugani
Akimalizia ziara yake katika kijiji cha Kakese Mkoa wa Katavi ametembelea katika Shule ya Sekondari Kakese na kutoa mifuko 27 iliyo na thamani ya shilingi laki 6 kuwezesha Ujenzi wa Maabara kuisha kwa haraka ili shule hio ianze kutumika kwani itawasaidia wanafunzi kusoma kwa uhuru.
Hata hivyo amewashauri wazazi kujitoa kuhakikisha wanamaliza Ujenzi wa Shule hio kwakutoa michango kwani Serikali inaunga juhudi zao pale wanapotia nia ya kufanya maendeleo na kuwataka kutowaozesha watoto katika umri mdogo kwani ni haki ya kila mtoto kupata Elimu
Anna ameonyesha ni namna gani anaunga mkono suala zima la Elimu na kutoa laki 5 kwa Mwanafunzi aliyehitimu kidato cha sita Rahel Jeremiah ili imsaidie kuendelea chuo kikuu na pia ameahidi shilingi laki 9 kwa vikundi vyote vilivyojitokeza katika zoezi zima la kukabidhi simenti hizo.
Baadhi ya wananchi wa kijiji cha kakese wamemshukuru kwa mchango wake kwani ni moja ya mambo ya msingi kama viongozi kuonyesha ushirikiano ili kuleta maendeleo katika jamii kwa kuunga juhudi za wananchi pale wanapoonyesha nia.
Takribani Tshg milioni 2 wananchi wamejitolea kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa maabara na kila kaya inatakiwa kutoa shg 2000 kwa ajili ya kumaliza ujenzi huo kwani watoto wao wanahangaika kusomea vijiji jirani hali ambayo inapelekea watoto kuwa na tabia hatarishi kwa kutopata malezi ya wazazi wao.
Aidha Wanafunzi waliojitokeza kupokea Seruji hizo wamemshukuru na kuwaomba Viongozi wengine kujifunza kwa Mbunge huyo ni mfano wa kuigwa kwani viongozi wanachaguliwa ili kutatua matatizo ya Wananchi na sio kujinufaisha wao