Watoto 8,082,838 kupatiwa Chanjo ya Surua-Rubella


Inakadiriwa  watoto wapatao  8,028,838 wenye umri wa miezi tisa hadi umri wa chini ya miaka mitano (miezi 59) wanatarajiwa kupatiwa chanjo ya Surua-Rubella kwenye kampeni shirikishi  ya chanjo itakayotolewa nchi nzima.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu wakati akizindua kampeni hiyo iliyofanyika  kitaifa mkoani hapa.

“Kampeni hii inaanza leo na itamalizika tarehe 21 mwezi huu na itatolewa bila malipo tanzania bara na itaendeshwa katika vituo vya kutolea huduma za afya na vituo maalam vitakavyoundwa na kubainishwa na halmashauri katika kipindi hiki ili kusogeza huduma karibu na walengwa”. Alisema Waziri Ummy Mwalimu.

Aidha, kwa upande wa kuzuia ugonjwa wa kupooza kwa watoto wenye umri wa mwaka mmoja na nusu  hadi miaka mitatu na nusu, Waziri huyo alisema inakadiriwa kuwa watoto  4,041,934 watapata chanjo hiyo.

“Lengo kuu ni kushiriki  katika mkakati wa kitaifa wa kutokomeza ugonjwa wa surua na rubella ili kuchangia katika kupunguza vifo vya watoto  hapa nchi,Zoezi hili la kampeni linatarajiwa kugharimu takribani shilingi za kitanzania billion 11.9 sawa na dola za kimarekani milioni 4.59”.

Hata hivyo alisema kuwa chanjo  hupunguza gharama kubwa  ambazo familia na taifa kwa ujumla  lingetumia katika kutibu magonjwa  yanayozuilika kwa chanjo“kuna faida kubwa katika  uchumi wa taifa tunapowekeza kwenye chanjo,kwani imethibitishwa kwamba kila dola moja unawekeza kwenye chanjo unapata  faida ya dola kumi na sita”.

Naye Mwakili Mkazi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Dkt. Tigest Mengestu alisema kuwa Tanzania inatoa chanjo hii kwa asilimia 95 na hivyo kampeni hii inasaidia kuimarisha  afya za watoto nchini na kuwakinga na magonjwa yanayozuilika kwa chanjo.