Zarif: Jamii ya Kimataifa na Baraza la Usalama la UN linawajihiana na maamuzi muhimu


Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amezungumzia kikao cha jana cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kilichoitishwa kujadili azimio nambari 2231 la baraza hilo na kusema kuwa, jamii ya kimataifa inawajihiana na maamuzi muhimu.

Muhammad Javad Zarif ameyasema hayo baada ya kikao cha jana cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kilichoitishwa kujadili ripoti ya tisa ya Katibu Mkuu wa umoja huo kuhusu utekelezaji wa azimio nambari 2231 lililopasisha makubaliano ya kimataifa ya nyuklia ya JCPOA.

Matokeo ya kikako hicho yatakuwa na taathira kubwa katika suala la vikwazo vya silaha vilivyowekwa dhidi ya Iran ambavyo muda wake unamalizika tarehe 18 mwezi Oktoba kwa mujibu wa azimio nambari 2231 la Baraza la Usalama.

Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Iran jana usiku baada ya kuhutubia kikao hicho kilichofanyika kwa njia ya video aliandika katika mtandao wa Twitter kwamba: Je tutaheshimu utawala wa sheria au tutarejea katika kipindi cha sheria za mwituni?


Katika kikao cha jana cha Baraza la Usalama wanachama wote wa baraza hilo, isipokuwa Marekani, waliunga mkono kikamilifuu mapatano ya nyuklia ya JCPOA baina ya Iran na nchi za kundi la 4+1.  

Wanachama wa Baraza la Usalama pia wamekosoa sera za kujichukulia maamuzi ya upande mmoja za Marekani katika kuiwekea vikwazo Iran na vilevile kitendo cha Washington cha kujiondoa katika mapatano ya nyuklia ya JCPOA na kusisitiza kuwa, suala la kurefusha vikwazo vya silaha dhidi ya Iran kwa msingi wa madai yaliyotolewa na Marekani, linapingana na makubaliano ya JCPOA na kukiuka azimio nambari 2231 la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.