Mazungumzo ya amani yananukia Afghanistan

Serikali ya Afghanistan na kundi la wanamgambo la Taliban wanakaribia kuafikiana kuhusu mazungumzo ya amani baada ya wawakilishi wa makabila kuidhinisha kuachiwa huru wafungwa 400 walio kitovu cha mvutano kati ya pande mbili.

Azimio hilo limefikiwa mwishoni mwa mkutano wa siku tatu unaofahamika kama "loya jirga" unaowakutanisha viongozi wa kikabila na wawakilishi wa makundi mengine, mkutano ambao wakati mwingine huitishwa ili kutafuta majibu ya masuala tata.

Mjumbe mmoja wa mkutano huo amesema kwa lengo la kuondoa vizingiti vya kuanza kwa mazungumzo ya amani na kukomesha umwagaji damu, baraza hilo limeridhia kuachiwa huru kwa wafungwa 400 kama kundi la Taliban lilivyotaka.

 Orodha ya wafungwa hao inajumuisha wale wanaotuhumiwa kwa makosa makubwa ya jinai ikiwemo kushiriki kwenye mashambulizi yalowauwa maelfu ya raia wa Afghanistan na wageni.