HALMASAHAURI ya Wilaya ya Kisarawe, mkoani Pwani, imewataka wananchi wilayani humo kujitokeza kushiriki katika kambi maalumu ya madaktari bingwa inayotarajiwa kuanza Septemba 15 mwakaa.
Akizungumza, mkoani humo, juzi, Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Wilaya ya Kisarawe, Yona Kabata, alisema lengo la kambi hiyo ni kusaidia jamii inayoshindwa gharama za kuwaona kwa wakati madaktari bingwa wa magonjwa mbalimbali.
Alisema kambi hiyo itakayo hitimishwa Septemba 17 itahusu madaktari bingwa wa wanawake, mifupa, watoto, magonjwa ya ndani, koo, pua, masikio,mionzi na upasuaji.
“Itakuwa ni kambi ya siku tatu, hivyo ninawaomba wananchi wa Wilaya ya Kisarawe kutumia fursa hii muhimu kwa kujitokeza katika kambi hii,”alisema.
Alisema wananchi watawaona madaktari bingwa bila malipo na kupewa huduma zote za kibingwa.
Dk. Kabata,alieleza kambi hiyo itafanyika katika Hospitali ya Wilaya ya Kisarawe ambapo itawahusi wanchi wanao tumia kadi za Bima ya Afya na wasio tumia kadi hizo.
Alisema madaktari bingwa wanane wa Hospital ya Wilaya Kisarawe watatoa huduma za kibingwa kwa magonjwa hayo ya wanawake, mifupa, koo, pua, masikio, upasuaji, mionzi na magonjwa ya ndani.
“Wagonjwa wote wataofika na kubainika kuwa na uhitaji wa huduma za zaidi watafanyiwa uchunguzi, upasuaji na ushauri,’alisema.
Dk. Kabata alieleza kambi hiyo itakuwa kubwa kufanywa na madaktari bingwa wa hospitali hiyo mbali na kliniki za kawaida wanazofanya.
“Hii inaashiria kukua na kutanuka kwa hudama za kibingwa na kuzosogeza karibu na wananchi wanaoshindwa kumudu gharama za matibabu,”alisema.
Baadhi ya wanchi wilayani humo, wamepongeza uongozi wa hospitali hiyo kwa kuandaa kambi hiyo ambapo wamedai itawasaidia kwa kiasi kikubwa kupata huduma za kibingwa kwa ukaribu zaidi.
“Wakati mwingine ukifika hospitali changamoto inakuwa ni kumwona daktari bingwa. Tunashukuru uongozi wa Hospitali ya Wilaya ya Kisarawe kwa kuletea huduma za kibingwa bure,”alisema Husein Ali.

