Na John Walter-Babati
Serikali imetenga shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa Daraja la
Kinambichi katika mwaka wa fedha 2026, hatua inayolenga kuboresha mawasiliano
na kurahisisha usafiri kwa wananchi wa vijiji vya Gichameda na Magugu wilayani
Babati.
Akizungumza wakati akiwasilisha bajeti kwenye Baraza la
Madiwani la Halmashauri ya Wilaya ya Babati, Meneja wa Wakala wa Barabara za
Vijijini na Mijini (TARURA) Wilaya ya Babati, Mhandisi Aloyce Nombo amesema
daraja hilo lililopo kitongoji cha Kinambichi lina umuhimu mkubwa katika
kuunganisha mawasiliano ya vijiji hivyo, hususan kipindi cha mvua ambapo
usafiri hukumbwa na changamoto.
Awali, Diwani wa Kata ya Magugu Stanley Charles alihoji
kuhusu mpango wa ujenzi wa daraja hilo na kupatiwa ufafanuzi kuwa tayari fedha
zimetengwa huku maandalizi ya utekelezaji yakiwa yanaendelea.
Katika hatua nyingine, Mhandisi Nombo amesema bajeti ya
TARURA Babati kwa mwaka wa fedha 2026/2027 ni shilingi bilioni tatu, milioni
themanini na tano na elfu themanini (3,085,080,000), fedha zitakazotumika
katika ujenzi na matengenezo ya miundombinu ya barabara na madaraja wilayani
humo.
Aidha, mradi wa barabara ya Magara Maji Moto kuelekea Hifadhi
ya Taifa ya Ziwa Manyara umetengewa shilingi milioni 426, ambapo taratibu za
mwisho zinaendelea kukamilishwa kwa kushirikiana na World Bank ili kuruhusu
utekelezaji wa mradi huo kuanza wakati wowote kuanzia sasa.
Ujenzi wa miradi hiyo unatarajiwa kuchochea maendeleo ya
kiuchumi na kijamii kwa kurahisisha usafirishaji wa mazao, kuboresha
upatikanaji wa huduma za kijamii pamoja na kukuza shughuli za utalii na
biashara katika wilaya ya Babati.
0 Maoni