F WAKAZI MRUKI NA MSASANI WAILILIA SERIKALI DARAJA LA KUDUMU MTO FAHHAY | Muungwana BLOG

WAKAZI MRUKI NA MSASANI WAILILIA SERIKALI DARAJA LA KUDUMU MTO FAHHAY


Na John Walter-Babati

Wakazi wa mitaa ya Mruki na Msasani katika Halmashauri ya Mji wa Babati mkoani Manyara wameiomba serikali kuwajengea daraja la kudumu katika Mto Fahhay ili kuondoa hatari inayowakabili wanafunzi wa Shule ya Msingi Mruki wanaolazimika kuvuka daraja la mbao kila siku wanapoenda shuleni.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, wakazi hao wamesema daraja hilo la muda limekuwa likitumika kwa zaidi ya miaka mitatu, lakini kwa sasa limeanza kuwa hatari kutokana na baadhi ya mbao na miti iliyotumika kulijenga kuoza na idadi ya watumiaji kuongezeka.

Shule shikizi ya Msingi Mruki yenye takribani wanafunzi 200 ilianzishwa na Halmashauri ya Mji wa Babati kwa lengo la kupunguza umbali mrefu waliokuwa wakitembea wanafunzi kutoka mitaa ya Mruki na Msasani kwenda katika shule mama ya Msingi Msasani na Darajani.

Mwenyekiti wa Bodi ya Shule ya Msingi Mruki, Bakari Said, amesema licha ya daraja hilo kuwa mkombozi kwa wanafunzi kwa kipindi cha zaidi ya miaka mitatu, sasa limekuwa tishio kwa usalama wao hasa wakati wa msimu wa mvua.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Mruki, Abdilahi Rajabu, amesema daraja hilo ni kiungo muhimu kinachounganisha mitaa ya Sinai na Mruki, ambapo asilimia kubwa ya watoto kutoka maeneo hayo husoma katika shule hiyo shikizi ya Mruki.

Naye Mariam Hamis, mkazi wa Mruki, ameiomba serikali kuharakisha ujenzi wa daraja la kudumu ili kuwaepusha watoto na wakazi wa eneo hilo na hatari ya kuanguka mtoni wanapovuka.

Baadhi ya wanafunzi wa shule hiyo akiwemo Samia Issa Ramadhani na Halima Idd wamesema hulazimika kuvuka daraja hilo kila siku kwenda na kurudi shuleni, hali inayowatia hofu hasa wakati daraja linapokuwa na utelezi au kuharibika.

Aidha, Agostino Balohho, ambaye ni mlinzi wa Shule ya Msingi Mruki, amesema daraja hilo la mbao ni njia fupi inayotumiwa na wanafunzi kutoka Mtaa wa Sinai kufika shuleni na pia hutumiwa na wakazi wa Mruki kama njia ya mkato kwenda mjini Babati kufuata huduma mbalimbali.

Kutokana na hali hiyo, wakazi hao wameiomba serikali pamoja na wadau wa maendeleo kuwasaidia kujenga daraja la kudumu litakalohakikisha usalama wa wanafunzi na wananchi wanaolitumia kila siku.

 


Chapisha Maoni

0 Maoni