Hali ya usajili,utunzaji wa kumbukumbu ya vizazi Nchini bado hairidhishi


KUTOKANA na ongezeko la mahitaji na matumizi ya cheti cha kuzaliwa nchini, hali ya usajili na utunzaji wa kumbukumbu ya vizazi bado hairidhishi jambo linalosababisha serikali kukosa takwimu sahihi kwa ajili ya mipango mbalimbali ya maendeleo kwa Taifa ikiwemo elimu,afya na huduma nyengine za msingi .

Kaimu Kabidhi Wasii Mkuu na Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usajili Ufilisi na Udhamini (RITA) Emmy Hudson ameyasema hayo katika semina ya viongozi wa mkoa na wilaya zake kuhusu  usajili wa watoto walio na umri chini ya miaka mitano kilichofanyika katika ukumbi mkuu wa mkoa wa Tanga.

Hudson alisema alisema kwa mujibu wa takwimu ya sensa ya 2012 ni asilimia 13 tu ya wananchi wa Tanzania Bara waliosajiliwa na kupatiwa vyeti vya kuzaliwa hivyo kuifanya kuwa moja kati ya nchi zenye kiwango cha chini cha usajili barani Afrika.

"Hii ni changamoto ambayo serikali kupitia RITA kama Taasisi yenye dhamana ya Usajili wa matukio muhimu ya binadamu kwa kwa kushirikiana na wadau wengine tumechukua hatua stahiki kwa kuandaa mkakati wenye lengo la kukabiliana na changamoto hii" amesema Hudaon.

Hata hivyo amebainisha kwamba tayari hatua madhubuti zimechukuliwa ili kukabiliana na changamoto hiyo kwa kufanya maboresho ya ujumla ya mfumo mzima wa usajili chini ya mkakati wa kitaifa na kuboresha Usajili wa matukio muhimu ya binadamu na takwimu. 


Alisema mkakati huo umeandaliwa baada ya kufanyika kwa tathimini ya kina na kubaini mapungufu katika mfumo wa usajili uliopo huku akieleza mpango huo wa Taifa wa kuboresha usajili na matukio muhimu ya binadamu na takwimu umebeba mipango mbalimbali ya utekelezaji ikiwa ni ya muda mfupi na mrefu ukilinganisha na makundi makuu matatu yanayotokana na umri ili kufikia makusudio ya usajili.

Aidha alisema kundi la kwanza ni watoto wa umri chini ya miaka mitano ambapo serikali kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo imebuni mpango wa usajili na kutoa vyeti vya kuzaliwa kwa watoto wa kundi hilo.

“Tayari mpango huu unaendelea kutekelezwa katika mikoa kumi na sita ya Mwanza, Mbeya,Songwe,Iringa,Njombe,Geita,Shinyanga,Mtwara,Lindi,Mara,Simiyu,Dodoma,Singida,Morogoro,Pwani na Ruvuma na kuonyesha mafanikio chanya hivyo kikao hiki ni maandalizi ya kuanza utekelezaji katika mkoa wa Tanga “Alisema

Awali akizungumza wakati akifungua semina hiyo Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga (RAS) Judica Omari ambaye alimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Tanga Martine Shigella alisema maisha ya mwanadamu yanaanzia pale anapozaliwa hivyo basi tukio la kizazi maana yake ni kuongezeka kwa idadi ya watu katika jamii na Taifa kwa upande wao kama serikali inawakumbusha wajibu wa kutoa huduma mbalimbali kwa wananchi.

Alisema kwa mantiki hiyo usajili na upatikanaji, utunzaji wa kumbukumbu sahihi kila tukio jipya la kizazi linapotokea ni la msingi kuweza kutambulika kwani kufanya hivyo kutaweza kuwa na uhakika wa kuweka takwimu sahihi kwa wakati na kupunguza matumizi ya takwimu za makisio ambazo zote wanazifahamu changamoto zake.