Hatua ya Uturuki ya kutuma jeshi kaskazini mwa Syria


Uturuki imetangaza kuwa imetuma kundi jingine la kikosi maalumu cha jeshi la nchi hiyo katika eneo la Ras al Ain huko kaskazini mwa Syria.

Wizara ya Ulinzi ya Uturuki imetangaza kuwa, askari hao wametumwa kutoka kitongoji cha Silvan katika mkoa wa Diyarbakır ulioko kusini mwa nchi na kupelekwa eneo la Ras al-Ain mkoani al-Hasakah, kaskazini mwa Syria.

Tangu miaka miwili iliyopita jeshi la Uturuki lilivamia na kukalia kwa mabavu baadhi ya meneo ya kaskazini na kaskazini mashariki mwa Syria kwa kisingizio cha kupambana na ugaidi. Uvamizi huo umelaaniwa na raia na serikali ya Syria na vilevile jamii ya kimataifa.

Hatua hiyo ya Uturuki ya kutuma kikosi kingine cha jeshi katika ardhi ya Syria imechukuliwa baada tu ya mkutano wa viongozi wa nchi za Iran, Russia na Uturuki katika mchakato wa Mazungumzo ya Astana, ambapo wamesisitiza udharura wa kulindwa umoja wa ardhi ya Syria, mamlaka yake ya kujitawala na kutoingiliwa masuala ya ndani ya nchi hiyo.


Mchambuzi wa Kimarekani, Irina Tsukerman anaamini kwamba: Mradi wa Marekani wa kuwaunganisha pamoja Wakurdi wa Syria hautafanikiwa kutokana na hitilafu za kimsingi baina ya makundi ya Kikurdi, utegemezi wa kifikra wa makundi ya Wakurdi wa Syria kwa Wakurdi wa Iraq na Uturuki na upinzani mkali wa serikali ya Uturuki dhidi ya kuanzishwa kambi moja ya Wakurdi nchini Syria.

Katika upande mwingine mazungumzo ya Astana yalianza yapata miaka mitatu iliyopita yakizishirikisha nchi za Iran, Russia na Uturuki kwa shabaha ya kukomesha mgogoro wa miaka 9 sasa wa vita vya ndani vya Syria, na katika kipindi hicho sehemu kubwa ya ardhi ya Syria imekombolewa na kudhibitiwa na serikali, na kundi la kigaidi la Daesh limeangamizwa. Hata hivyo Uturuki ina wasiwasi kwamba, lengo la Marekani la kutaka kuitisha mazungumzo ya kuyaunganisha pamoja makundi ya Wakurdi na kudhoofisha serikali kuu ya Syria, litaimarisha msimamo wa Wakurdi na kutia nguvu madai yao ya kuanzisha utawala wa ndani.

Katika upande mwingine Uturuki inapeleka majeshi zaidi huko Syria kwa shabaha ya kuimarisha nafasi yake mkabala wa rais ajaye wa Marekani kabla ya uchaguzi wa rais wa nchi hiyo ambao matokeo yake hayajulikani na yumkini asiwe Donald Trump. Katika mkondo huo pia kuna uwezekano Uturuki ikazidisha mashambulizi yake katika jimbo la Kurdistan nchini Iraq na hata kuanzisha kambi mpya za jeshi katika eneo hilo.


Alaa kulli hal, yanayoshuhudiwa kwa sasa katika eneo la magharibi mwa Asia hayadhamini maslahi ya Uturuki wala Syria, na hapana shaka kuwa utawala wa Kizayuni wa Israel na Marekani zinataka kufaidika na hali hiyo. Uturuki pia inapaswa kuitambua vyema kwamba, ple inaposaini hati katika mikutano ya Astana, Sochi, Tehran na Ankara inalazimika kuheshimu hati hizo la sivyo jambo hilo litakuwa na madhara kwa Waturuki wenyewe na linaweza kuteteresha amani na utulivu wa kanda nzima ya magharibi mwa Asia