Rais Samia Suluhu aahidi ushirikiano CCM na kusimamia maadili

 


TUTASHIRIKIANA! Ndiyo kauli ya Mwenyekiti mpya wa Chama cha Mapinduzi CCM ambaye pia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan mara baada ya kuthibitishwa kuwa Mwenyekiti mpya wa Chama hicho.

Rais Samia amethibitishwa kuwa Mwenyekiti wa Sita wa CCM leo jijini Dodoma akipigiwa kura za ndiyo zipatazo 1,862 kati ya kura halali 1,862 ikiwa ni asilimia 100 ya kura zote.

Akizungumza baada ya kutangazwa kuwa Mwenyekiti mpya, Mama Samia amesema licha ya kufahamu kazi aliyokabidhiwa siyo nyepesi lakini anaamini kwa uzoefu alionao anatosha na anaweza kuifanya kwa weledi na uwezo mkubwa.

Mama Samia amesema kwa miaka 20 ya kuwa Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM anafahamu kuwa changamoto zinazowakabili watendaji wa ngazi za Mikoa na Wilaya ikiwemo ya usafiri ambapo ameahidi kuyatatua kwa kushirikiana na wanachama wa CCM.

" Ninafahamu kuna changamoto za uhaba wa vitendea kazi kama usafiri kwenye Wilaya zetu na Mikoa yetu jambo ambalo linalofifisha utendaji kazi wa kukijenga chama chetu na Nchi yetu kwa ujumla.

Changamoto nyingine ni maslahi duni kwa watendaji wetu pamoja na malimbikizo ya madai ya stahiki ikiwemo ya uhamisho na kustaafu, niwaahidi nitashirikiana nanyi katika kutatua changamoto hizo kwa pamoja, " Amesema Rais Samia.

Rais Samia pia amesisitiza kusimamia maadili, kanuni na taratibu za chama hicho ili kuweza kufanya kazi kwa weledi katika kuwatumikia watanzania na wanachama wa CCM.

Katika mkutano huu pia imeshuhudiwa Mwenyekiti wa CHADEMA Kanda ya Kati na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama hicho Lazaro Nyalandu akitangaza kukihama chake na kurejea CCM.

Post a Comment

0 Comments