"Hakuna Uhamisho kwa Mtumishi aliyeharibu kwenye kituo chake cha kazi” Mhe. Ummy


Nteghenjwa Hosseah, Chemba

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Ummy Mwalimu(Mb) amesema mtumishi wa Tawala za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa atakayeharibu katika kituo chake cha kazi hataruhusu ahame isipokua atamuwajibisha akiwa katika kituo chake cha kazi.

Waziri Ummy ameyasema hayo katika ziara yake Wilayani Chemba Mkoani Dodoma kukagua miradi ya maendeleo na kuzungumza na Kamati ya Fedha  pamoja na Menejimenti ya Halmashauri  hiyo tarehe 04.05.2021.

“Sitaruhusu  mtumishi aharibu Chemba kisha ahamishiwe Kongwa, niwahakikishie kuwa ntamshughulikia akiwa hapa hapa Chemba na nikibaini ana hatia ntamchukulia hatua stahiki” alisema Mhe. Ummy.

Aliongeza kuwa Watumishi wa Mamlaka za  Serikali za Mitaa walizoea kufanya ubadhirifu wa miradi ya maendeleo haswa ya Elimu, Afya na Barabara na wakishaona mradi haujakamilika au unatuhuma hizi na zile anahama sio wakati wa Uongozi wangu hakuna atakayehama kukwepa tuhuma.

“Na hapa Chemba wote waliohama sababu ya kutokukamilisha miradi ya maendeleo kama Ujenzi wa Hospitali ya Wilaya watarudi  kuja kujibu tuhuma zao” Alisisitiza Mhe. Ummy.

Waziri Ummy yupo katika ziara za kukagua miradi ya maendeleo na kuzungumza  na kamati za Fedha za Halmashauri ya Wilaya ya Chemba, Bahi na kongwa.

Post a Comment

0 Comments