Mkoa wa Njombe bado watajwa kukabiliwa na ukatili mkubwa katika jamii, UWT wajitwisha zigo


Na Amiri Kilagalila,Njombe

Usiri mkubwa katika familia na imani za kishirikina zinatajwa kuongeza kiwango cha ukatili kwa wanawake na watoto mkoani Njombe unaofanywa kwa siri na vitisho.


Afisa ustawi wa jamii mkoa wa Njombe Theresia Yomo katika mkutano wa baraza la wanawake wa UWT ccm wilaya ya Njombe amesema bado mkoa wa Njombe ungali na matukio ya ukatili wa kutisha ukiwemo ubakaji,ulawiti,vipigo pamoja na familia kuingiliana kwa imani za kishirikina.Huku jumuiya ya wanawake wa CCM wilaya ya Njombe wakiahaidi kuendelea kushirikiana ili kutokomeza matukio ya ukatili wilayani humo


“Usirikina hapa bado ni mkubwa sana kuna wamama wanalawitiwa na waume zao ili biashara ziende vizuri na tumeshuhudia wengi wanapata matatizo na hizi kesi tunazo ofisi”alisema Theresi Yomo


Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Njombe mzee Edward Mgaya amesema wanawake hao wanapaswa kuzingatia malezi mema kwa watoto wao ili kuwafundisha maadili yatakayosaidia kupunguza ukatili katika siku za usoni.


“Ukiangali kwenye vyombo vya habari kuna watu wanafanya vitu vibaya sana dhidi ya watoto pia,hili ni lazima tuliangalie sana na tuwe makini”alisema Mgaya


Baadhi ya wananchi mkoani Njombe akiwemo Tumeitwa Sanga ametaka kupatiwa ushirikiano wa haraka pindi matukio ya ukatili yanapotokea kwani kumekuwa na kusuasua hasa vyombo vya dola.


Kila pahala nchini raia wanapaswa kuendelea kupaza sauti juu ya kupinga vitendo vya ukatili ambao unafifisha ndoto za watoto wengi ambao wanakumbwa na kadhia hizo.

Post a Comment

0 Comments