Tanzania kushiriki mkutano wa 26 wa nchi Wanachama wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu mabadiliko ya tabianchi

Tanzania inatarajiwa kushiriki Mkutano wa 26 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi utakaofanyika kuanzia Novemba mosi hadi 12, 2021 mjini Glasgow nchini Uingereza.

Hayo yamebainika leo Juni10, 2021 wakati wa kikao kati ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Selemani Jafo na Balozi wa Uingereza nchini Tanzania, Mhe. David Concar aliyemtembelea ofisini kwake jijini Dodoma leo Juni 10, 2021.


Waziri Jafo alisema kuwa mkutano huo utakaofanyika utatoa mchango mkubwa katika sekta ya mazingira kwani nchi mbalimbali zitakutana na kujadili namna gani ya kuchangia kupambana na mabadiliko ya tabianchi, kupunguza hewa ya ukaa duniani na ukataji wa miti.

Alimpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kukuza uhusiano wa kidiplomasia na nchi mbalimbali na ambazo zimekuwa zikitoa mchango katika hifadhi ya mazingira.

“Changamoto ya mazingira imekuwa ni kubwa kwa hiyo ni jukumu letu Ofisi ya Makamu wa Rais inayosimamia Sera na kuratibu shughuli zote za mazingira na kuhakikisha nchi yetu inakuwa kinara katika uhifadhi mazingira,” alisema Jafo.

Pia aliwaomba wadau mbalimbali na wananchi kwa ujumla kuungana kwa pamoja na kuifanya Tanzania kuwa ya mfano katika mapambano dhidi ya mabadiliko ya tabianchi yanayoikabali nchi yetu.


Katika mazungumzo yao, Balozi Concar alipongeza juhudi mbalimbali zinazofanywa na Serikali ya Tanzania kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais hususan katika kuhakikisha suala la uhifadhi na usafi wa mazingira linakuwa endelevu.

Balozi huyo aliahidi kuwa nchi yake itaendelea kutoa ushirikiano kwa Tanzania katika kupambana na mabadiliko ya tabianchi ambayo yamekuwa yakisababisha madhara kwa binadamu yakiwemo ukame na mafuriko.

Alisema mkutano huo utakaofanyika Uingereza utakuwa na mchango mkubwa kwa kuwa nchi mbalimbali zitakutana na kujadili namna gani ya kuchangia katika kupambana na mabadiliko ya tabianchi na kupunguza hewa ya ukaa duniani na ukataji wa miti.

Kikao hicho kilichohudhuriwa pia na Mkurugenzi wa Mazingira, Dkt. Andrew Komba pamoja na Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Mazingira, Bi. Catherine Bamwenzaki Akizungumza na Balozi Concar.

 

Post a Comment

0 Comments