Umoja wa Ulaya waunga mkono wito wa Biden kwa uchunguzi zaidi juu ya chanzo cha virusi vya corona


Umoja wa Ulaya umetilia mkazo wito wa Marekani wa kufanyika uchunguzi wa kina kuhusu kiini cha virusi vya corona, hatua ambayo inaweza kuighadhibisha China.Rais wa Halmashauri Kuu ya Umoja wa Ulaya Ursula von der Leyen leo hii amewaambia waandishi wa habari, siku moja kabla ya kuanza kwa mkutano wa kilele wa viongozi wa mataifa ya kundi la nchi saba zilizoendelea zaidi kiuchumi duniani, G7 huko Uingereza, kwamba ni muhimu wajifunze kuhusu asili ya virusi vya corona.

Nae Rais wa Baraza la Ulaya, Charles Michel alipoulizwa kama umoja huo utaunga mkono wito wa Biden wa kufanyika uchunguzi zaidi alisema uwazi unahitajika na ulimwengu una haki ya kuelewa ni kitu gani hasa kimetokea. 

Baada ya utafiti uliofanywa na Shirika la Afya duniani WHO, katika eneo la jimbo la Wuhan, la China ambalo kirusi hicho kiligundulika kwa mara ya kwanza Desemba 2019, wataalam walisema virusi hivyo vilitoka kwa wanyama na kuambukizwa binadamu.

 Lakini wajuzi wanasisitiza bado kunahitajika utafiti zaidi.

Post a Comment

0 Comments