Mambo ya kuzingatia kabla ya kuchagua jina la Biashara

 

Uteuzi wa jina la biashara ni hatua muhimu kama ilivyo kwa jiwe la pembeni katika nyumba. Watu wengi wamekuwa hawatilii maanani mambo muhimu ya kuzingatia wakati wa kuchagua jina la biashara au kampuni.

Nimekuwa nikishuhudia makapuni mengi yakitumia majina ya ajabu ajabu yasiyoendana na biashara zao. Kwa sehemu kubwa kufanikiwa na kujulikana kwa biashara yako kunategemea jina la biashara yako.

Fuatana nami katika makala hii ambayo nitakueleza mambo kadhaa ya kuzingatia kabla ya kuchagua jina la biashara.

1. Uhusiano wa jina na bidhaa au huduma
Je unafahamu kwamba jina la biashara linatakiwa liakisi huduma au biashara unayoifanya? Ni jambo jema kutumia jina linaloakisi kile unachokifanya. Kwa mfano jina kama vile “Muungwana electro” lifaa kwa kampuni ya vifaa vya kielektroniki, “Pamba LTD” lifaa kwa kampuni ya upambaji au mavazi.

Itakuwa ni jambo la kushangaza kutumia “Muungwanaelctro” kwenye mavazi au kutumia “Pamba LTD” kwenye vifaa vya kielektroniki. Ukizingatia hili mapema utaweza kuitambulisha bidhaa au huduma yako vyema kwa kupitia jina la biashara yako.

2. Jina fupi linalovutia na kueleweka
Uchaguapo jina la la biashara au kampuni yako kaa chini tafuta jina fupi lenye mvuto na linaloeleweka.

Usitumie majina magumu na marefu kama vile “matunda bora ya shamba”, “rextymyshoes” “mauaborasana”, “John Noe na Rose Mewa Beauty Saloon”, n.k. Chagua jina fupi linalovutia ambalo pia ni rahisi kwa watu kulikumbuka.

3. Zingatia mahitaji ya kimtandao
Katika swala hili nimeshuhudia watu wengi wakichukua majina ya biashara au kampuni bila kujali swala la matumizi ya mtandao. Kwa mfano mtu anaweza kusajili kampuni inayoitwa hope, smart, green nk.

Majina haya huwezi kuyatumia kwenye mtandao kwani tayari yameshatumika katika mambo mengi sana; hapa hutoweza kupata huduma kama vile anwani ya tovuti au baruapepe inayoendana na jina la kampuni yako.

Hivyo basi tumia huduma kama vile (Whois) kutazama kama unaweza kupata anwani ya matandao inayoendana na jina la kampuni au laa.

Kumbuka haina maana kampuni kuitwa Moja LTD halafu ikawa na tovuti inayoitwa “http://mbili.com”; hapa utapoteza watu, hawataweza kuifikia tovuti yako vyema.

4. Upekee
Kama nilivyoeleza katika hoja zilizopita hapo juu ni muhimu kuhakikisha unabuni jina lenye upekee kwa ajili ya biashara yako. Epuka kutumia majina yanayofanana na majina mengine.

Kumbuka zipo shereia za kimataifa zinazolinda majina ya kibiashara (Brands) za kampuni mbalimbali; majina kama vile Microsofti, Thetoyota, Delli, Vodacomu n.k yatakupelekea kuingia kwenye mgogoro wa kisheria na makampuni husika kwani majina haya yanalandana sana na majina ya kampuni zao.

5. Zingatia mahitaji ya baadaye
Inawezekana jina la kampuni au biashara linalofaa leo lisifae tena kwa ajili ya biashara yako baadaya ya miaka mitano. Hivyo ni vyema kuchagua jina ambalo utadumu nalo katika kampuni yako.

Kwa mfano mtu akiita kampuni yake 3GNetworks au 4GNetworks, baada ya miaka mitano 3G na 4G kwenye jina hazitakuwa za maana tena kwani tutakuwa tayari tuna teknolojia mpya za 5G n.k.

Hivyo ni muhimu kuzingatia kuwa jina unalolichagua leo litakufaa pia kwa upanuzi na matumizi ya baadaye ya biashara yako.

Kwa kuhitimisha ninapenda kukushauri kuzingatia umakini na utafiti wa kutosha katika kuchagua jina la biashara yako. Hakikisha kama unahusisha watu wengine katika machakato huu wawe ni wale wanaoilelewa vyema biashara au kampuni yako.

Post a Comment

0 Comments