Mambo ya kuzingatia kabla ya kujiingiza katika mahusiano ya kimapenzi

 

Mapenzi ni moja ya mahitaji muhimu ya wanadamu, kila mmoja wetu ahahitaji kupenda na kupendwa, hapo hamna majadiliano ndio jinsi tulivyoumbwa. Katika enzi za mababu zetu, watu walikuwa wanaishi kwa raha, amani na upendo japokuwa walikuwa wanachagulia wake au waume wa kuishi pamoja kama mke na mume, enzi hizo zimepitwa na wakati siku hizi watu wanajitafutia wenza wao wenyewe, ila siku hizi watu ndio hawana amani, ndoa zinavunjika kila siku na wanaobakia kuteseka zaidi ni watoto ambao wanaishia kuishi bila mama na baba.

Ukweli ni kwamba inachukua muda mrefu kumfahamu mtu vizuri, kikubwa zaidi watu wanabadilika jinsi wanavyokuwa, hela zinaongezeka au kupungua na wanajikuta wanavutiwa na watu wa aina tofauti. Kwa wale ambao hawajabahatika kupata wenza wao kuna mambo ya msingi ya kuzingatia kabla hujajizamisha katika dimbwi la mapenzi, ukizingatia mambo haya, hata kama mtu uliyenaye atabadilika , uwezekano wa kuvumiliana na kuweza kuishi pamoja ni mkubwa zaidi.

1. ni lengo (ambition),
kama mmoja kati wa wapenzi (nazungumzia wapenzi ambao wanampango wa kuishi pamoja kama mke na mume) ni mtu wa kuwa na malengo na anataka kufanya kitu fulani au kuwa mtu fulani katika maisha yake na mwenzake anachukulia siku kama inavyokuja (laid back), huyu ambaye ana malengo atamchukulia ambaye ni “laid back” kama ni mvivu. Wapenzi wanatakiwa wasipishane sana katika malengo yao hata kama wana kazi mbali mbali.

2. ni uwazi (openness), 
kama mpenzi wako ni “open minded” anapenda kujifunza vitu tofauti, kujaribu vyakula tofauti, kusafiri n.k. Yule ambaye anapenda kujifunza mambo mapya kila siku atamuona mwenzake anaboa.

3. wapenzi wanaweza kuwa tofauti katika ujuzi wa hisia (emotional intelligence). 
Hapa kama tofauti sio kubwa, watu wanaweza kuvumiliana na kuishi pamoja, ila kama tofauti ni kubwa sana, yule ambaye hana ujuzi wa hisia, atakuwa anamburuza na kumharibia mudi yule ambaye amesimama imara kwenye mambo ya hisia. Onyo kwa wanaume ambao wana ujuzi au utaalam wa kusoma hisia za wanawake, wanawake ambao wana F katika ujuzi wa hisia huwa wanavutiwa sana na watu kama ninyi.

4.  ni usosho,
kama mmoja wenu ni mtu wa watu anapenda kuongea na watu na anamarafiki kibao, utamkwaza ambae ni mtu ambaye anapenda maisha “private” na ya utulivu. Mwenzako atakuwa bize anaweka picha zenu na status zinazowahusu facebook wakati wewe unataka mambo ya ndani yawe ya ndani tu. Kama tofauti si kubwa sana mnaweza vumiliana kama tofauti ni kubwa, muda si mrefu mtashindwana

5.  ni wivu.
Wivu ni kitu kibaya sana, kama mpenzi mmoja ana wivu ni ngumu kuekewana na ambaye hana wivu. Kama wote mna wivu, sawa kwani kila mmoja ataepuka kufanya mambo ambayo yanamuumiza mwenzake, ila kama mmoja ndio ana wivu ataona mwenzake hajali, basi ukimuona mwenzako anaongea na classmate wake wa zamani au ukiona mtu amepiga picha na mpenzi wako ameshikwa bega basi inakuwa fujo tupu. Kama upo tayari kwenye uhusiano, na mwenzako ana wivu, jaribu kumuelewesha kwamba kum-kumbatia rafiki yako sio kwamba ndio una mipango mingine ya siri.

Kikubwa katika yote ni uaminifu, kama hamna uaminifu katika mapenzi au ndoa. Usipasue kichwa, ondoka na tafuta mtu ambaye anakuamini au kama haupo tayari kuwa mwaminifu usijiingize katika mahusiano, utajiumiza mwenyewe na mwenzako. Msome mwenzako kabla ya kuanza kuitana wachumba, kama tangu siku ya kwanza mwenzako ana wasiwasi na wewe ukikaribia simu yake, ni afadhali umuulize mapema, kulikoni? Kama umepoteza uaminifu katika mahusiano yako, usihofu, muonyeshe mweza wako kwamba umebadilika na jinsi muda unavyoenda atajifunza kukuamini tena.

Hizi sifa zilizotajwa hapo juu sio za kina sana, lakini ni moja wapo ya mambo ya kuzingatia katika kuchagua mwenza wako wa maisha(kama basi mapenzi yana macho) kabla ya kujizamisha katika mapenzi. Je wewe unaona ni mambo gani ya kuzingatia katika mahusiano na ni mambo gani yanasababisha ndoa kuvunjika? Usisite kuandika maoni yako.

Post a Comment

0 Comments