https://monetag.com/?ref_id=TTIb RUNALI yafanya mnada wa mwisho wa korosho, bei ya juu shilingi 1,721 | Muungwana BLOG

RUNALI yafanya mnada wa mwisho wa korosho, bei ya juu shilingi 1,721


Na Ahmad Mmow, Nachingwea. 

Chama kikuu cha ushirika cha RUNALI mkoani Lindi, leo kimefunga msimu wa ununuzi wa korosho kwa msimu wa 2021/2022 kwa kuuza tani 395 na kilo 77 za korosho ghafi. 


Katika mnada huo wa kumi na moja kwa msimu wa 2021/2022 uliofanyika mjini Nachingwea bei ya juu ya korosho daraja la kwanza ni shilingi 1,721, na bei ya chini ni shilingi 1,660 kila kilo moja. Huku mahitaji ya wanunuzi yalikuwa kilo 1,650,212. 


Kwa mujibu wa meneja mkuu wa RUNALI, Jahida Hassan katika mnada huo kulikuwa na barua sita za wanunuzi walioomba kununua korosho hizo zilizopo katika maghala ya Export, Lindi farmers, Halmashauri ya wilaya ya Nachingwea, Lipande, Hassan Mpako na Umoja. 


Jahida alisema katika ghala la Export kuna tani 23 na kilo 64, Lindi farmers tani 78 na kilo 954, Halmashauri ya wilaya ya Nachingwea tani 38 na kilo 876, Lipande tani 35 na kilo 352, Umoja tani 165 na kilo 818 na Hassan Mpako tani 53 na kilo 13. 


Aidha meneja mkuu huyo wa RUNALI alisema katika mnada huo ambao ni wa 18 kwa vyama vikuu vya ushirika vilivyo katika mkoa wa Lindi kulikuwa korosho daraja la pili ambazo zimenunuliwa kwa bei ya shilingi 1,300 kila kilo moja.  


Alizitaja kampuni zilizofanikiwa kununua korosho hizo kuwa ni Doman, Thabita na VNBP. 

Post a Comment

0 Comments