Wazazi wanaosomesha watoto wao China wapewa darasa

Wazazi  na walezi wenye nia ya kuwasomesha  watoto wao  China wameshauriwa  kutumia njia sahihi za kuwasiliana na vyuo ikiwemo ubalozi wa nchi yao ili kulipa ada moja kwa moja  kwa ajili ya kuhakikisha wanafunzi wanapokelewa bila utapeli.

Mkurugenzi wa Kampuni ya  Soma China Consulting and Service Co.Limited, Ru Lin amesema  hayo  jijini hapa kuwa baadhi ya wazazi na walezi wamejikuta  wakitumia fedha nyingi kwaajili ya kupeleka watoto China wakati wanaweza kutumia gharama nafuu na kuwawezesha watoto wao kupata elimu bora.

Amesema  kutokana na changamoto hiyo kampuni hiyo imeandaa maonyesho ya vyuo vikuu tisa vinavyotoa elimu katika sekta mbalimbali yatakayofanyika Shule ya Sekondari Arusha kwa siku tatu ambayo yatafunguliwa na Katibu Tawala wa mkoa wa Arusha,Richard Kwitega .

“Baadhi ya Watanzania wamekua wakipata changamoto ya kutumia fedha nyingi kwaajili ya kupata wakala wa kumwezesha kupata vyuo vizuri wanavyotaka lakini ni vyema wanatumia Ubalozi wetu hapa nchini kwaajili ya kujua aina za vyuo vikuu vilivyopo China na kiwango cha ada ili kuepuka udanganyifu,”amesema  Ru

Amesema  licha ya nchi yao kupiga hatua kubwa kimaendeleo wanahimiza  nchi mbalimbali ikiwemo Tanzania  kutumia njia sahihi za kupata vyuo vinavyotoa elimu nzuri ambayo itawasaidia wahitimu baadaye na kuwataka kuhudhuria maonesho hayo.

Kwa upande wake ,Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Arusha, Christopher Malamsha amewataka  wazazi na walezi kufika kwenye maonesho hayo ili kufungua fursa za elimu kwa watoto wao badala ya kutumia gharama kubwa kutafuta vyuo kwa njia zisizo rasmi.

Amesema kuwa elimu ni msingi bora katika  maisha ya kila mwanadamu hivyo elimu bora inatokana na mzazi  alivyowekeza kwa mtoto wake na  kuwa maonyesho hayo ya vyuo vikuu tisa kutoka  China yatatoa fursa ya kujifunza.
Mpya zaidi Nzee zaidi

Popular Items