https://monetag.com/?ref_id=TTIb Magufuli na Kenyatta waahidi kuimarisha uhusiano | Muungwana BLOG

Magufuli na Kenyatta waahidi kuimarisha uhusiano

Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta na mwenzake wa Tanzania Dkt John Magufuli wamekutana mjini Kampala, Uganda na kuahidi kuimarisha uhusiano kati ya nchi hizo mbili.

Wawili hao wamewaagiza mawaziri wa nchi hizo mbili kutatua tofauti ndogondogo zinazojitokeza katika biashara kati ya nchi hizi mbili.

Marais hao wametoa maagizo hayo walipokutana hoteli ya Munyonyo mjini Kampala muda mfupi kabla ya kuanza kwa vikao vya mkutano wa wakuu wa nchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Uhusiano kati ya nchi hizo mbili ulikuwa umeonekana dorora wiki za karibuni hasa kutokana na hatua ya Tanzania kuwakamata na kuwateketeza vifaranga kutoka Kenya na pia kuwapiga mnada ng'ombe wa watu wa jamii ya Wamaasai kutoka Kenya.

Wawili hao wamesema wanataka kuona biashara kati ya Tanzania na Kenya inazidi kukua na bidhaa zinauzwa na kununuliwa baina ya nchi hizo bila vikwazo vyovyote na hivyo kuagiza tofauti zilizojitokeza katika baadhi ya bidhaa zimalizwe.

"Kuna mambo madogomadogo yanakuwa yanajitokeza katika biashara kati ya Kenya na Tanzania, tunataka kwa haya yote Mawaziri wa Kenya na Mawaziri wa Tanzania mkae myatatue, sisi hatuna tatizo, mambo mengine madogomadogo mno, mambo ya viatu, nguo, ngano, gesi ni madogo sana, mnatakiwa myatatue nyinyi yasifike kwetu, sisi huku tuko sawasawa" amesema Dkt Magufuli, tamko ambalo limeungwa mkono na Bw Kenya.

Wametoa maagizo hayo kwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wa Tanzania Dkt. Augustine Mahiga, Waziri wa Katiba na Sheria wa Tanzania Prof. Palamagamba Kabudi upande wa Tanzania.

Upande wa Kenya, maagizo yametolewa kwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Kenya Balozi Monica Juma na Waziri wa Afrika Mashariki na Maendeleo ya Ushoroba wa Kaskazini wa Kenya Peter Munya.