Wahamiaji haramu wakamatwa Iringa

Idara ya Uhamiaji kwa kushirikiana na Polisi Mkoa wa Iringa wamewakamata wahamiaji haramu wanne raia wa Ethiopia waliokuwa katika basi wakisafiri kutoka Namanga mkoani Arusha wakielekea Afrika Kusini kupitia nchini Malawi.

Kamishna msaidizi mwandamizi wa uhamiaji  Mkoa wa Iringa, Hope Kawawa  amesema leo Februari 22, 2018 kuwa wahamiaji hao walikamatwa maeneo ya Kituo Kikuu cha Mabasi Iringa Mjini  saa nne leo na maofisa wa uhamiaji kwa kushirikiana na polisi, hivyo wanaendelea kuwahoji.

Kawawa amesema kwa sasa Iringa si mahala pa kupitisha wahamiaji, hivyo  wataendelea kuwakamata na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria kwa sababu askari wapo kazini kwa saa 24.

“Naomba niwaambie madalali wanaosafirisha hawa wahamiaji, Iringa siyo mahala salama kabisa kuwapitisha hao watu kwani tuko makini na tukiwabaini wahusika hatua kali zitachukuliwa dhidi yao,” amesema.

 Aliwataja wahamiaji waliokamatwa kuwa ni Ayano Kabede Manamo, Mesfin Leimengo, YonasNiguse Legbo na Mamush Gatuso Kidre ambao wawili walikutwa na pasipoti bila kuwa na viza ya kuwaruhusu kuingia nchini.

Alisema idara ya uhamiaji inaendelea kufanya uchunguzi baada ya wahamiaji hao kubainika kuandika majina ya uongo katika tiketi za basi walilopanda, ambalo kutokana na uchunguzi kuendelea alikataa kulitaja.


Mpya zaidi Nzee zaidi