UEFA yaja na mabadiliko haya

Shirikisho la soka Barani Ulaya (UEFA) limezifanyia mabadiliko baadhi ya kanuni zinazosimamia michuano ya ngazi ya vilabu iliyochini yake ambayo ni (Champions League ) pamoja na (Europa League). Kanuni mpya zitaanza kutumika msimu ujao wa 2019/20.

Moja ya kanuni kubwa ambayo itaanza kutumika msimu ujao kwenye michuano ya Ligi ya Mabingwa ni timu zitaruhusiwa kufanya mabadiliko (Sub) ya nne endapo mechi itaenda "Extra Time" katika hatua ya mtoano.

Kuanzia msimu ujao katika mechi za Fainali klabu Bingwa Ulaya, Fainali Europa League na UEFA Super Cup, jumla ya wachezaji 23 watajumuishwa kwenye kikosi ambapo 11 wataanza huku 12 wakiwa benchi. Hii imewekwa kwa lengo la kuwapa makocha nafasi kubwa ya kuchagua wachezaji katika mechi hizo muhimu.

Awali kanuni hiyo ilikuwa inaruhusu wachezaji 18 pekee kujumuishwa kwenye mchezo, 11 wakianza na 7 wakiwa benchi ambapo sasa kuanzia msimu ujao itakuwa ni hivyo hivyo katika mechi zote isipokuwa mechi za Fainali.

Pia UEFA imefanya mabadiliko kwenye kanuni ya usajili, ambapo timu zitaruhusiwa kusajili wachezaji wapya watatu baada ya mechi za makundi bila ya vizuizi vyovyote, hivyo makocha watapata uhuru zaidi katika usajili wa dirisha la januari kwasababu wachezaji watakaowasajili watawatumia bila kujali wamecheza michuano hiyo.

Msimu huu Arsenal imeshindwa kumtumia Pierre-Emerick Aubameyang kwenye mechi za Europa League kutokana na mchezaji huyo kuichezea Borrusia Dortmund. Pia Barcelona imeshindwa kumtumia Philippe Coutinho kutokana na kuichezea Liverpool kwenye michuano hiyo.