Chuo cha Royal College na vingine 20 vyafungiwa na Nacte



Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (Nacte) limefuta usajili wa vyuo 20 baada ya kushindwa kufuata sheria zinazoendana na matakwa ya usajili wa vyuo hivyo.

Akizungumza leo Juni 8, Kaimu Katibu Mtendaji wa baraza hilo Dk Adolf Rutayuga amesema uamuzi huo umefikiwa baada ya kufanyika kwa ukaguzi wa vyuo 458 na 32 vilikutwa na mapungufu.

Sanjari na 20 vilivyofungiwa vyuo tisa vimezuiliwa kudahili wanafunzi wapya huku vyuo vitatu vikitakiwa kusitisha baadhi ya kozi walizokuwa wakitoa bila idhini ya baraza.

Dk Rutayuga amesema tayari baraza hilo limeshaviandikia barua vyuo 20 vilivyofungiwa kuvitaka vihakikishe kuwa wanafunzi wanahamia kwenye vyuo vingine.

Vyuo vilivyofutiwa usajili ni Royal College, Covenant College of Business Studies,  Mugerezi Spatial Technology College, Techno Brain, Lisbon Business College, PCTL Training Institute na Mlimani School of Professional Studies vyote vya Dar es Salaam.

Vingine ni Regency School of Hygiene, St Peters College of Health Sciences, Genesis Institute of Social Science, Institute of Management and Information Technology na Boston City Campus of Business College.

Vingine ni Arusha Institute of Technology, East African Institute of Enteprenuership and Financial Management (Arusha) Iringa RETCO Business College (Iringa) na Musoma Utalii College (Musoma).

Vipo pia Highlands Health Institute (Njombe),  Institute of Social Work na Dinobb Institute of Science and Business Technology (Mbeya).