Maisha yazidi kumnyookea Hamisa Mobeto, apata dili nono

 Maisha yameanza kumnyookea mwanamitindo Hamisa Mobeto kwa kuvuna kweupee shilingi milioni 5.7 kwa mwezi (zaidi ya milioni 60 kwa mwaka) leo Agosti 8, 2018, baada ya kuingia mkataba wa mwaka mmoja wa kuwa balozi wa kiwanda kinachotengeneza nywele (rasta) cha Prima Afro, kilichopo Tabata, Matumbi jijini Dar.

Kwa mujibu wa chanzo ambacho ni rafiki wa karibu na mwanamitindo huyo, waandaji waliangalia ni mtu gani anaweza kuwatangaza zaidi miongoni mwa mastaa na kuona Mobeto anafaa zaidi yao.

“Amewapiga bao mastaa wenzake wengi, ama kweli mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni, Mobeto hivi karibuni amesemwa sana mitandaoni, kuanzia kipindi cha ile bethidei ya mtoto wake, Daylan hadi hii ya juzijuzi na Zamaradi, kumbe Mungu alikuwa na mipango naye, ona sasa amevuna mkwanja mrefu,” kilisema chanzo.

 Chanzo kiliendelea kumwaga data kuwa, Mobeto ameingia mkataba kwa njia ya dola ambapo amelipwa kiasi cha dola za Kimarekani 2,500.

“Hajataka tu kusema ni mkataba wa kiasi gani lakini ni dola za Kimarekani ambapo sasa ukichukulia dola 2,500 kwa pesa za Kibongo ni kama shilingi milioni 5.7 hiyo ni kwa mwezi, ukifanya kwa mwaka mmoja alioingia atakuwa amevuna kiasi cha shilingi milioni 68.4 kwa nini asiwe na kismati ikiwa wenzake hawajavuna pesa hizo ndani ya mwaka huu,” kilitia nukta chanzo hicho.

Mara baada ya kusaini mkataba huo, Mobeto alisema kuwa, hakujua lakini kumbe walikuwa wakimchunguza nguvu yake kwenye mitandao ya kijamii.

“Baada ya kunichunguza, walinifuata ofisini kwangu tukazungumza, nikausoma mkataba na kuangalia masharti yao na kiwango wanachotaka kunilipa niliporidhia tukapanga siku ambayo ni leo nikasaini,” alisema Mobeto.