UN yataka kuachiwa huru mwanaharakati Nabeel Rajab

Mwanaharakati Nabeel Rajab

Bodi ya umoja wa mataifa UN,imetaka kuachiliwa huru kwa mwanaharakati wa haki za binadamu wa Bahraini Nabeel Rajab aliyefungwa kwa madai ya kufanya makosa ya kueneza habari za uongo na kukashifu mamlaka za kiserikali.

UN inasema kuwa hukumu ya Nabeel Rajab ilifanyika kinyume cha sheria na ilikiuka uhuru wake binafsi wa kujieleza.

Hadi sasa Nabeel amekwisha tumia miaka mingi tu gerezani tangu alipokuwa akiongoza harakati zake za kidemokrasia mwaka 2011.Lakini serikali kwa upande wake inasema kuwa mashitaka ya Rajab yalitolewa katika mfumo wa uhuru na uwazi.

Nabeel Rajab, mkuu wa kituo cha haki za binadamu cha Bahrain Center for Human Rights (BCHR) na makamu katibu mkuu wa taasisi ya kimataifa ya haki za binadamu ya International Federation of Human Rights (FIDH), amekuwa akishikiliwa tangu june mwaka 2016.

Mwezi Februari mwaka huu alihukumiwa kifungo cha miaka mitano jela kutokana na kutoa ujumbe kupitia ukurasa wake wa Twitter ulikuwa ukipinga kile kinachodaiwa kuwa ni mateso wanayoyapata wafungwa wa Bahrain na vitendo viovu vya jeshi la Saudia wakishirikiana na muungano wa wapiganaji wa vita vya wenyewe kwa wenyewe vya Yemen

Hata hivyo hukumu hiyo ilikuja huku akiwa anatumikia kifungo cha awali cha miaka miwili gerezani baada ya kukutwa na makossa ya kueneza habari zinazodaiwa kuwa ni za uongo.

Shirika la Human Rights Watch limesema kuwa taarifa kutoka kwa wanafamilia wa Rajab,zinasema kuwa anaishi katika mazingira magumu,anafungiwa katika chumba kichafu,chenye wadudu ambacho ukubwa wake si zaidi ya futi kumi,lakini pia afya yake imedhoofu na anasumbuliwa na ugonjwa wa ngozi ambapo anahitaji matibabu.