Hatimaye mwaka 2018 ndio huo unaelekea mwishoni kabisa,
umekuwa na mambo mengi kwa kiasi chake kwenye kila nyanja.
Kwa upande wa burudani ni mengi yamejiri na kutikisa
vilivyo. Haya ni matukio 10 yaliyotawala upande wa Burudani kwa mwaka huu.
1.
Kifo cha Masogange
Ni binti mrembo aliyejulikana kama Agnes Gerald kutoka
mkoani Mbeya. Mara baada ya kutokea kwenye video ya muimbaji Belle 9
'Masogange' akiwa kama video vixen ndipo alipata umaarufu mkubwa na kuanza
kutumia jina hilo.
Hata hivyo Masogange alianza kuonekana kwenye video ya
wimbo wa Mwana FA na AY inayokwenda kwa
jina la Nangoja Ageuke iliyotoka mwaka 2008. Baada ya kuonekana kwenye video za
wasanii kadhaa na kujizolea umaarufu mkubwa aliamua kuingia kwenye filamu.
Hatimaye April 20, 2018 katika Hospitali ya Mama Ngoma
iliyopo Mwenge, Dar es Salaam, Masonge alifariki dunia akiwa ni mama wa mtoto
mmoja na kuzikwa April 23, 2018 mkoani Mbeya.
Mwili wa Masogange uliagwa April 22, 2018 katika
viwanja vya Leader Club, Da es Salaam.
Katika misa/ibada hiyo iliyohudhuriwa na idadi kubwa ya wasanii kulitokea
matukio mawili ambayo yalijadiliwa sana
kwenye mitandao ya kijamii.
Mosi; Kukutana kwa Alikiba na Diamond, hawa ni wasanii
wakubwa Tanzania ni washindani kwenye muziki wao. Kitendo cha Alikiba kumgeuzia
kiganja wakati wakusalimia kiliweza kujadili sana.
Pili; Ni
muigizaji Rammy Galis ambaye alikuwa ni mpenzi wa Masogange kuzimia na kubebwa
na watu lakini aliendelea kung'ang'ania na kushikilia kitambaa chake cha mkononi,
wengi walidai kitu hicho hakiwezekani.
Kabla ya umauti kumfika, April 03, 2018 Masogange
aliachiwa huru na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam baada ya
kukutwa na hatia ya kutumia dawa za kulevya aina ya Heroine na Oxazepam
(alilipa faini).
2.
Harusi ya Alikiba
Alfajiri ya April 19, 2018 (alhamisi) Alikiba alifunga
ndoa na Mrembo Aminah Rikesh Ahmed huko mjini Mombasa nchini Kenya. Kama
ulikuwa hujui siku kama hiyo miaka mingi iliyopita ndipo na wazazi wa muimbaji
huyo walifunga ndoa.
Baada ya Mombasa, shughuli nzima ikahamia Dar es Salaam
ambapo Aprili 29, 2018 kwenye Hoteli ya Serena maharusi hao walijumuika na watu
wao wa karibu na wageni waalikwa.
Harusi hiyo ilikuwa ikijadiliwa sana mtandaoni na wengi
waliweza kuishuhudia moja kwa moja kupitia Azam TV.
Miongoni mwa watu maarufu waliohudhuria ni pamoja na
Mke wa Rais Mstaafu, Mama Salma Kikwete, Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu, Waziri
wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamisi Kigwangalla na wengineo.
Pia siku hiyo ndio kwa mara ya kwanza Alikiba
alitambulisha kinywanji chake cha Mofaya ambacho pia kwa mara ya kwanza
kilionekana kwenye wimbo wake uitwao Mvumo wa Radi kwa lengo la kukitangaza
(product replacement).
Pia ndani ya mwezi huo (April 22, 2018) mdogo wake na
Alikiba, Abdu Kiba naye alifunga ndoa ambapo walifanya sherehe ya harusi pamoja
ndani ya Serena Hotel kama nilivyotangulia kueleza.
3.
Video ya Faragha ya Nandy na Bill Nass
Kwa kipindi kirefu walikuwa wakizushiwa kuwepo
mapenzini lakini walikuwa wakitupilia mbali tetesi hizo zilizowanyima usingizi wapenda udaku.
Hatimaye mchana wa April 12, 2018 ikabainika ni kweli
Nandy na Bill Nass waliwahi kuwa wapenzi baada ya video yao wakiwa faragha kuvuja
mtandaoni.
Hadi kufika Aprili 17, 2018 suala hilo lilifika bungeni
ambapo Mbunge wa Ulanga, Goodluck Mlingwa aliyehoji jinsi gani serikali
imejipanga kupambana na wasanii wa muziki
anaosambaza lugha za matusi.
Akijibu swali hilo Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa
na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe alisema siku moja kabla Diamond Platnumz
alikamatwa kwa kosa hilo na kutoa agizo kwa polisi kumkatamata na Nandy.
Hata hivyo siku mbili mbele (April 19, 2018) Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA)
iliwaita Nandy na Diamond kwa ajili ya mahojiano ambapo wote walikiri makosa
yao na kupewa nafasi ya kuomba radhi.
Diamond alijikuta kwenye sekeseke hilo kufuatia pia
kuvuja kwa video yake ya faragha akiwa na mzazi mwenzie, Hamisa Mobetto na
wanawake mwingine mmoja ambaye hakufahamika.
Hilo pia halikumuacha salama Hamisa Mobetto kwani naye
pamoja na Irene Uwoya, July 19, 2018 waliitwa na Kamati ya Maudhui ya Mamlaka
ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) na
kuwataka kuomba radhi kwa kosa la kuweka picha za utupu mtandaoni ambapo
walitii hilo.
4.
Kuteuliwa kwa Jokate Mwegelo
Mrembo huyo aliyekuwa Miss Tanzania namba mbili mwaka
2006 alitambulika vema akiwa kama Mwanamitindo, msanii wa muziki na filamu, pia
mjariamali.
Mchana wa July 28, 2018 Rais John Magufuli alimteua kuwa
Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe. Uteuzi wake ulikuwa baada ya mrembo huyo kususia
mitandao ya kijamii tangu April 20, 2018 hadi kipindi cha uteuzi kwa sababu
ambazo yeye binafsi hajawahi kuziweka wazi.
Kabla ya uteuzi huo Jokate aliwahi kuwa Kaimu Katibu wa
Hamasa na Chipukizi wa Umoja wa Vijana Chama cha Mapinduzi (UVCCM), kabla ya
March 25, 2018 Mwenyekiti wa umoja huo, Kheri Denis James kutangaza kutenguliwa
kwa uteuzi wake.
Ijumaa ya August 03, 2018 ndipo Jokate aliapishwa na
Rais wa Jahmuri wa Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli kuanza kutumikia
nafasi hiyo.
Uteuzi wa Jokate ulipokelewa kwa shangwe na vijana
wengi kutokana na nguvu ya ushawishi alionayo kwao kwa kipindi kirefu.
Utakumbuka May 2017 Jokate Mwegelo alichaguliwa na
jarida la Forbes Africa kuwa miongoni mwa vijana 50 wenye umri chini ya miaka
30 waliopata mafanikio katika sekta mbalimbali.
5.
Kifo cha Mzee Mjuto
Jina alilopewa na wazazi wake ni Amri Athuman, sanaa ya
maigizo na uchekeshaji ikampa jina la Mzee Majuto. Alifanikiwa kuvunja mbavu za
mashabiki wake kwa miaka ya mtoto hadi mtu mzima (zaidi ya 18).
Usiku wa Augusti 08, 2018 ndipo alifariki dunia akiwa
anapatiwa matibabu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) mara baada ya
kutoka nchini India.
Kabla ya umauti kumfika, Mzee Majuto alipatiwa matibabu
ndani na nje ya nchi ambapo May 04, 2018 alisafirishwa kwa ajili ya matibabu
nchini India na June 22, 2018 alirejea nchini.
Mzee Majuto aliagwa August 09, 2018 kwenye viwanja vya
Karimjee, Dar es Salaam na tukio hilo kuhudhuriwa na Rais John Magufuli, Rais
Mstaafu Jakaya Kikwete na viongozi wengine, alizikwa siku iliyofuata mkoani
Tanga.
6.
Muendelezo wa Wasafi Festival, Miss Tanzania na SZIFF
Tunaweza kusema kwa mwaka huu kulikuwa ni kupatwa kwa
wapenda Burudani mara baada ya kurejea kwa kishindo kwa Wasafi Festival na
shindano la Miss Tanzania.
Tamasha la Wasafi chini ya Diamond Platnumz na wasanii
wote wa WCB liliwahi kufanyika na kusitishwa na mwaka huu limerejea ambapo
limeweza kupita kwenye mikoa ya Mtwara, Morogoro, Iringa, Mwanza, Sumbawaga na
Visiwani Zanzibar.
Hapo awali WCB waliwahi kufanya Wasafi Festival lakini si
kwa ukubwa wa sasa. Utakumbuka tena walifanya kitu kinaitwa Wasafi Beach Party,
hii ikiwa ni katika jitihada za kuandaa show zao wenyewe.
Tuakiachana na hilo, pia mwaka huu yamereja mashindano
ya Miss Tanzania baada ya kutofanyika kwa miaka miwili.
Utakumbuka baada ya kufanyika mwaka 2016 na mrembo
Diana Edward kuibuka mshindi yalisimama hadi yalipokuja kufanyika mwaka huu na
mrembo Queen Elizabeth kuibuka mshindi.
Pia mwaka huu ugawaji wa tuzo za filamu za Sinema Zetu
International Film Festival Awards (SZIFF) uliendelea ambapo ulifanyika April
01, 2018 kwenye ukumbi wa Mlimani City, Dar es Salaam.
Tuzo hizo zilikuwa na jumla ya vipengele 18 huku kimoja
kikiwa cha People Choice na kukamilisha jumla ya vipengele 19, mgeni rasmi alikuwa Rais Mstaafu Jakaya Kikwete.
Muigizaji Gabo Zigamba aliondoka na tuzo tano, huku Wema
Sepetu akijinyakulia mbili.
Kitendo cha Diamond na Hamisa Mobetto kuonekana pamoja
jukwaani ni kitu kilichowavutia wengi kwa sababu ndio ilikuwa mara ya kwanza
kuoneka pamoja baada kupata mtoto na kuibua figisufigisu (drama) za hapa na
pale.
Pia ujio wa muigizaji wa tamthilia kutoka nchini India,
Pritika Rao ulinogesha vilivyo tuzo hizo na kuweka historia ya aina yake kwa
wapenda burudani nchini.
(namba
hii imekuwa na matukio matatu kwa sababu ni yenye kujirudia).
7.
Kifo cha Patrick
Mtoto Patrick Dickson aliwavutia wengi kwenye mitandao
ya kijamii, ni mtoto wa msanii wa filamu Bongo, Rose Alphonce Nungu maarufu
kama Mona Love.
Patrick alifariki July 03, 2018 nchini Kenya akipatiwa matibabu ambapo
alikuwa akisumbuliwa zaidi na maradhi ya miguu hali iliyo mpelekea kushindwa
kutembea na mara kadhaa alifanyiwa upasuaji.
Masikini, ni Patrick maarufu kama Patda Smart Boy,
habari za kifo chake zilizombaa zaidi mtandaoni. BBC Swahili kupitia mtandao
wao walichapisha habari kuhusu 'malaika' huyo aliyeonekana kuja kufanya vizuri
kwenye uimbaji na mitindo.
8.
Diamond na BASATA
Kwa mwaka huu Diamond Platnumz amekuwa na wakati mgumu
zaidi kwa upande wake na Baraza la Sanaa Taifa (BASATA) baada ya nyimbo zake kadhaa
kufungiwa.
February 28, 2018 Mamlaka ya Mawasiliana nchini (TCRA)
ilipokea orodha ya nyimbo 15 zisizokuwa na maadili kutoka Basata ambazo
zilifungiwa na kutotakiwa kuchezwa kwenye vyombo vya habari.
Kati ya hizo ni nyimbo mbili za Diamond ambazo ni Waka
na Hallelujah. Kufuatia hatua hiyo Diamond alijikuta 'akivutana' kimaneno na
Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Juliana Shonza.
Katika mahojiano na kituo cha Radio Times FM, Mach 19,
2018, Diamond alimshtumu Shonza kuwa anafanya uonevu kwa kufungia nyimbo zake
na hana uelewa kuhusu sana.
Kutokana na hilo kitu hicho cha Radio ilipofika March
22, 2018 kiliandikiwa barua na TCRA kikitakiwa kuwasilisha kipindi cha The
Playlist kilichorushwa tarehe hiyo kwa uchunguzi zaidi.
Baada ya hilo kutulia Diamond akajikuta tena Basata,
safari hii lilikuwa ni suala la msanii Rich Mavoko aliyekuwa akitaka kujitoa
kwenye lebo hiyo kwa kile kinachodaiwa ni mkataba wa kinyonyaji ingawa hilo
limekuwa likakanushwa na pande zote mbili.
August 09, 2018 kuliibuka taarifa kuwa Rich Mavoko
ameshinda kesi ya kujitoa WCB ndipo zikaanza safari za muimbaji huyo na uongozi
wa lebo hiyo Basata kwa lengo la kusuluhishi. hata hivyo hadi mwisho jitihada
hizo hazikufua dafu.
Baada ya hilo kupita, ilipofika November 12, 2018 wimbo
wa Rayvanny na Diamond 'Mwanza' ulifungiwa na Basata kutokana kukiuka maadili.
Ilipofika December 18, 2018 wasanii hao wakafungiwa kutojihusisha na sanaa kwa
muda usiojulikana kutokana na kuendelea kuutumia wimbo huo.
9.
Babu Seya na Papii Kocha jukwaani tena
Kwa zaidi ya miaka 13 mashabiki walikuwa wamekosa
burudani ya wasanii wao waliotamba vilivyo miaka ya nyuma. Ni Nguza Viking ‘Babu Seya’ na mwanaye Johnson Nguza ‘Papii Kocha’ waliokuwa
wakitumikia kifungo jela.
Kwa mara ya kwanza March 10, 2018 Babu Seya na Papi
Kocha walifanya show ya pamoja ndani ya ukumbi wa King Solomon Hall, Dar es
Salaam.
Utakumbuka December 09, 2017 wakati Tanganyika
ikihadhimisha miaka 56 ya Uhuru, Rais Dkt. John Magufuli alitoa msahama kwa
wasanii hao.
Mwaka huu ndipo waliweza kuonekana vilivyo uraiani na
kwenye matukio mbalimbali ya sanaa. January 02, 2018 walifika Ikulu kwa ajili
ya kumshukuru Rais Magufuli, pia April 19, 2018 walialikwa Bungeni na Spika wa Bunge, Job Ndugai.
10.
Lulu uraiani
Utakumbuka November 13, 2017 muigizaji wa filamu Bongo,
Elizabeth Michael ‘Lulu’ alihukumiwa kifungo cha miaka miwili jela baada ya
kukutwa na hatia ya kumuua aliyekuwa muigizaji mwenzake, Steven Kanumba bila
kukusudia.
Usiku wa May 12, 2018 zikaanza kusambaa stori kuwa Lulu
ameonekana uraiani, siku iliyofuta Jeshi la Magereza lilieleza kuwa Lulu
amebadilishiwa adhabu na atatumikia kifungo cha nje kwa amri ya Mahakama Kuu ya
Tanzania, Dar es Salaam.
Hatimaye Jumatatu ya November 12, 2018 Lulu akamaliza
kutumikia kifungo chake cha nje na kuwa raia huru.
Kesi ya Lulu ilianza kunguruma tangu mwaka 2012 ambapo
ndipo kifo cha Kanumba kilitokea, mwaka 2013 alitoka kwa dhamana hadi pale
ilipokuja tena kusikilizwa mwaka 2017 na hukumu kutolewa.
Imeandikwa
na Peter Akaro











