Huduma za dharura na mahututi zazinduliwa Hospitali ya rufaa Tanga


Wakazi wa Jiji la Tanga sasa wataanza kupata huduma za uhakika za dharura pamoja na huduma za wagonjwa mahututi katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga (Bombo).


Huduma hizo zimefunguliwa rasmi leo na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu wakati ziara yake ya siku mbili mkoani humo huku akiwahakikishia wananchi wa Tanga kutolazimika kupewa rufaa kwa ajili ya kufuata huduma hizo Muhimbili na KCMC.


"Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli inaendelea kuboresha huduma za afya katika Hospitali za mikoa kwa kujenga jengo la huduma za dharura lililogharimu Tsh. Milioni 211.6 na jingo la kuwahudumia wagonjwa mahututi Tsh. Milioni 350 katika kipindi cha mwaka 2018/19," amesema Waziri Ummy.

Waziri Ummy ameongeza kuwa kuanzishwa kwa huduma hizo za dharura na mahututi zitatatua changamoto zilizokuwepo katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga na kuongeza kuwa katika kipindi cha mwaka 2018/19 Serikali iliipatia Hospitali hiyo ya Mkoa Tsh. Milioni 200 kwa ajili ya ujenzi wa mtambo wa kutengeneza Oksijeni (Oxygen Implantation).

 Aidha, Waziri Ummy amesema kuanzishwa kwa huduma za dharura na mahututi zinategemewa kupunguza vifo vitokanavyo na dharura kwa asilimia 50, huku akiongeza kuwa Serikali inatarajia kuhakikisha kuwa dawa zinapatikana kwa asilimia 100 Hospitalini hapo, kutengeneza lifti katika wodi ya Galanos, kujenga kituo cha uchunguzi na vipimo pamoja na kujenga jengo la tiba shufaa kwa wateja walioathirika na matumizi ya madawa ya kulevya.

Pamoja na hayo Waziri Ummy ameishukuru Taasisi ya ABBOTT chini ya makamu wake wa Rais Bw. Andy Wilson kwa kusaidia ukarabati wa jengo la huduma za dharura kwa wagonjwa pia Waziri amewashukuru Wafanyabiashara wa Mkoa wa Tanga kwa kuchangia kuboresha huduma za afya katika Hospitali hiyo.