Mambo 9 yanayochangia maisha marefu katika ndoa


Inasemekana maisha katika ndoa si kitu rahisi kwani kuna changamoto nyingi na tofauti. Inasemwa kwamba hakuna kanuni inayojulikana ambayo unaweza ukaifuata na kufanikiwa kwa kuwa kila ndoa inachangamoto tofauti sana.

Watalamu wa saikologia hata hivyo wamefanya tafiti kadhaa na kuja na viashiria ambavyo unaweza kuvitumia kujua uhai au uimara wa ndoa kati ya wenza wawili. Majibu ya tafiti zao ambazo zimefanyika nchini Marekani ni za kushangaza ila za kusisimua kama ambavyo ninaziandika katika makala hii.

Ushahidi unaonesha kuwa muda wa uchumba,utofauti wa umri kati ya wenza,kipato cha familia,imani ya dini, uzuri wa umbo au kipato kama kigezo cha kuchagua mchumba ni baadhi ya mambo yanayochangia maisha marefu katika ndoa au kinyume chake.

1. Muda wa Uchumba
Wanandoa ambao wametumia muda mrefu katika uchumba angalau miaka mitatu wana nafasi kubwa zaidi ya kutoachana ukilinganisha na wale wanaokaa uchumba kwa muda mfupi zaidi. Sababu zinaweza kuwa katika muda mfupi huo wanakuwa hawajapita zile hatua zinazofaa kujenga upendo wa kweli.


2. Utofauti wa Umri wa Wanandoa
Ni jambo la kushangaza lakini ndivyo utafiti unavyoonesha kuwa utofauti mkubwa wa umri kwa wanandoa unaongeza uwezekano wa kuachana.

Wanandoa wenye umri unaokaribiana zaidi wana nafasi ndogo ya kuachana au kugombana.

3. Kipato cha Familia
Familia yenye kipato kikubwa ina nafasi kubwa ya kuishi kwa muda mrefu. Kinyume chake ni kuwa ndoa ambazo hali ya kipato ni mbaya ina uwezekano mkubwa zaidi kwa wanandoa kuachana.

Unaweza ukaangalia hali ya maelewano kati ya wanandoa wakati wakiwa katika uchumi mbaya. Ni wazi magomvi yanaongezeka sana.

4. Ukubwa wa Harusi
Matokeo mengine ya kushangaza ni kuwa hata ukubwa wa harusi unachangia kwa maana ya idadi ya watu walioalikwa katika harusi. Harusi iliyoshuhudiwa na watu wengi zaidi hudumu sana ukilinganisha ile ambayo haikuwa na watu wengi walioshuhudia. Mbaya zaidi ni ile ambayo wanandoa wawili tu wanashiriki.

Sababu inaweza kuwa ukishudiwa na watu wengi unapata tabu kufanya maamuzi ya kuachana kwani unahisi kuwaeleza kila mtu kuwa mmeachana na mwenza wako ni kitu kigumu na hivyo kuendelea hata kama hakuna amani na furaha.

Tunajua kuwa kuna ndoa nyingi zinaishi katika hali hii. Hofu ni kwamba watu wataonaje na watasemaje.

5. Gharama za Harusi
Harusi za kifahari au zile ambazo ni za gharama kubwa zina nafasi kubwa kwa wanandoa kuachana baadae. Sababu yake kubwa haiko wazi ila inaweza kuwa sababu za vigezo vya watu hawa kuchaguana si za kudumu. Labda ni kwasababu ya mali kigezo ambacho si cha kudumu.

6. Uumini na Uhai katika Dini
Wanadoa ambao wote ni waumini katika dini na wanashiriki ibada na mafundisho wana nafasi ndogo ya kuachana. Dini nyingi zinakazia watu kuvumiliana na kutoachana hivyo ni wazi wanaishi kwa hofu ya Mungu. Wanatumikia ‘Pingu za Maisha’ kama zinavyoitwa.

7. Mwonekano wa Mwenza
Hii inawaathiri wanaume zaidi kuliko wanawake. Wanaume ambao wanaamua kumuoa mchumba kutokana na mwonekano mzuri wa umbo kama kigezo cha msingi mara nyingi wana nafasi kubwa ya kuachana na wenza wao katika ndoa.

Kigezo cha umbo ni dhaifu katika maamuzi ya ndoa labda kama kuna vigezo vingine vinavyosaidia. Kwani mwonekano mzuri huisha au kuchuja.

8. Kipato cha Mwenza
Hii inawaathiri wanawake zaidi kuliko wanaume. Uamuzi wa kuolewa na mtu mwenye kipato kikubwa cha fedha kama kigezo kikubwa mara nyingi husababisha ndoa kuvunjika kwa kuwa kipato si kigezo cha kudumu. Siku kipato kikipungua na maisha kuwa magumu mtazamo unaweza ukawa tofauti na kupelekea matatizo katika ndoa.

Japo kipato ni muhimu lakini si kigezo pekee katika kujenga mahusioano ya kudumu.

9. Kwenda Fungate
Wanandoa ambao wanaenda fungate kwa namna ya kushangaza wanaonekana kuwa na nafasi ndogo ya kuachana kuliko wale wasioenda au walioenda kwa muda mfupi.

Sababu labda ni kuwa fungate linawajenga katika mapenzi zaidi na inaweka kumbukumbu ya siku zao za furaha kwa muda wote wa maisha yao.

Kama nilivyosema awali kuwa hakuna kanuni maalumu za kufuata na kuishi kwa furaha katika ndoa lakini mambo haya yanatoa mwanga juu ya vitu vya msingi ambavyo vinaonekana katika mahusiano mengi ya ndoa na huenda vikasaidia kwa wanandoa wapya na hata wakongwe na hasa wachumba katika kufanya mabadiliko katika mahusiano yao ili kujenda familia itakayodumu daima.

Je uko katika mahusiano? Nini uzoefu wako?. Naomba ushiriki kutoa maoni hapa chini yanayoelimisha na kujenga juu ya mambo yanayochangia maisha marefu katika ndoa.