Tanroads yatoa sababu ya ubomoaji Barabara ya Morogoro


      Dar es Salaam. Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) umesema kutofautiana kwa mita zinazotumika katika ubomoaji nyumba zilizoko kuanzia eneo la Ubungo na Kiluvya, kunatokana na Sheria ya Hifadhi ya Barabara ta Mwaka 1932 na mipango ya Serikali.

Tanroads imesema sheria hiyo inataja umbali tofauti wa hifadhi ya barabara katika baadhi ya maeneo na imeendelea kuwa mwongozo kwa Barabara ya Morogoro.

Nyumba zinazobomolewa kati ya Ubungo na Kimara ziko ndani ya mita 90 kutoka katikati ya barabara, wakati zilizobomolewa kutoka Kimara Stop Over hadi Kiluvya ziko ndani ya mita 121.9.

Akizungumza na Mwananchi jana, kaimu mkuu wa Idara ya Mipango Tanroads, mhandisi Elson Mwelanzi alisema tofauti hiyo inatokana na mipango ya Serikali.

“Katika sheria hii iliyoanza eneo la Faya hadi Ubungo ni mita 22.5, kutoka Ubungo hadi Kimara Mwisho ni mita 91.7 na kutoka Kimara Stop Over hadi Kiluvya ni mita 121.9 hayo ndiyo maeneo ya hifadhi ya barabara,” alisema Mwelanzi.

Alisema sababu ya Kimara Stop Over hadi Kiluvya kuwa na umbali wa mita 121.9 ni kutokana na mpango wa Serikali wa kuwa na hifadhi kubwa ya barabara.

“Hii sheria ilibadilishwa katika maeneo mengine mwaka 1967 na baadaye mwaka 2000, lakini katika hifadhi ya Barabara ya Morogoro haijawahi kubadilishwa. Sababu mojawapo ni kwamba hii ni barabara kuu hapa nchini,” alisema.

Alisema sheria hiyo ni nzuri kwa sababu inapunguza gharama za malipo kwa wakazi waliojenga ndani ya hifadhi.

“Ujenzi ndani ya hifadhi ya barabara unasababisha miradi kuwa na gharama nyingi si tu kwa ajili ya ujenzi, bali pia kulipa wakazi waliovamia maeneo,” alisema.

“Nakumbuka watu walilalamika na wakashauri sheria hii ibadilishwe, lakini mimi sishauri hii ibadilishwe ibaki kwa sababu watu hawatajenga ndani ya hifadhi ya barabara na miundombinu itapangwa vizuri,” alisema.