Diamond, Ali Kiba wapata wapinzani mpya

Wasanii Sultan King kutoka Zanzibar na Rapa mkongwe Msafiri Diouf wamesema ujio wao mpya utawafanya mashabiki wa muziki nchini kuacha kuwazungumzia mastaa wawili Diamond Platnumz na Ali Kiba.

Diouf ambaye aliwahi kutamba na Bendi ya Twanga Pepeta kabla ya kutimkia nchini Uingereza amesema yeye na Sultan King wamejipanga kuhakikisha wanaleta mapinduzi makubwa katika tasnia ya muziki nchini.

" Hatujaja kushindana na mtu lakini wimbo wetu wa fire fire utawaonesha mashabiki sisi ni watu wa aina gani, letu ni kuwa na akina Diamond na Ali Kiba 80 ili kuweza kuiletea sifa na heshima Tanzania sio kila siku wasanii ni wale wale," alisema Diouf.

Kwa upande wake, Sultan King alisema ameshafanya kolabo nyingi na wasanii wakubwa akiwemo Ali Kiba, Ben Pol huku akiweka wazi kuwepo na mpango na Bosi wa WCB, Diamond wa kufanya kazi pamoja.

" Zipo kazi nyingi sana tumeshafanya na wasanii wakubwa kilichopo na kuachia tu ili mashabiki waweze kufaidi matunda ya muziki mzuri, ukiachilia kolabo za nyumbani zipo pia za kimataifa kutoka Nigeria ambazo siwezi kuziweka wazi kw sasa," alisema Sultan King.