Mamlaka ya hali ya hewa yatoa tahadhari mpya

Mamlaka ya hali ya hewa iliyopo chini ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano nchini Tanzania imewatahadharisha wananchi kuwepo kwa vipindi vya mvua kubwa na upepo mkali unaozidi km 40 kwa saa katika maeneo yote ya pwani kuanzia saa 24 zijazo kutoka sasa.

Hayo yamebainishwa na taarifa zilizotolewa na mamlaka hiyo jioni ya leo (Jumatatu) na kudai kutakuwepo vipindi vya mvua kubwa katika saa 24 ambavyo vinatarajiwa katika maeneo ya mkoa wa Morogoro, Dar es Salaam, Pwani, Tanga Lindi, Mtwara pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba.

Mbali na hilo, TMA imesema kuna tarajiwa vipindi vifupi vya mvua kubwa vinavyotarajiwa katika baadhi ya maeneo ya mikoa ya Kagera, Mwanza, Mara, Simiyu, Kigoma, Dodoma, Singida, Kilimanjaro, Arusha na Manyara huku upepo wa pwani unatarajiwa kuvuma kutoka kusini kwa kasi ya km 40 kwa saa kwa Pwani yote.