Salah: kutwaa UEFA ndio kitu muhimu kwangu

Nyota wa Liverpool Mohamed Salah anaamini rekodi alizoweka Anfield hivi sasa hazina maana kuliko kuchukua ubingwa wa UEFA Champions League.

Salah amefikisha jumla ya mabao 30 msimu huu akiwa mchezaji wa kwanza kutoka Afrika kufanya hivyo baada ya kufunga bao moja kati ya matatu ambayo Liverpool ilishinda dhidi ya Bournemouth.

Mmisri huyo ameeleza kwa sasa wanapaswa kuweka nguvu kubwa katika kupambania taji la Ligi ya Mabingwa Ulaya huku akisema mbio za kuwania ufungaji bora kwenye ligi hauna maana yoyote kwake.

"Kama ningeweza kuchagua kati ya kuwania kiatu cha mfungaji bora na taji la UEFA, kwangu ningechagua UEFA. Kushinda taji hilo ni kitu kikubwa zaidi kwangu, hayo mengine hayana maana" amesema Salah.