Waandamanaji 240,000 Hong Kong watimuliwa na Polisi nje ya Bunge


Maelfu ya wakaazi wa Hong Kong wamefanya maandamano mjini humo jana kuupinga mpango wa serikali utakaoruhusu watuhumiwa kupelekwa China bara kukabiliwa na mashtaka.

 Wakati maandamano hayo yalikuwa ya amani kwa kiasi kikubwa, mamia kadhaa ya waandamanaji walikabiliana na polisi nje ya bunge la mji huo jana jioni.

Makundi madogo ya waandamanaji yaliahidi kupiga kambi nje ya bunge hadi Jumatano, wakati mswada huo unaolalamikiwa utakaposomwa kwa mara ya pili bungeni.

Hata hivyo, walifurushwa na polisi wakati kibali chao cha kuandamana kilipomalizika muda wake usiku wa manane. Tukio hilo lilikuwa mojawapo ya maandamano makubwa kabisa katika historia ya Hong Kong, ambapo polisi walikadiria kuwa karibu waandamanaji 240,000 walishiriki. Lakini waandaaji wa maandamano hayo walisema karibu watu milioni moja walishiriki.