Viongozi wa upinzani wameahidi kusimamisha mgombea mmoja wa urais mwaka 2027. Hata hivyo, bado hawajamteua, huku kila mmoja akikabiliwa na mtihani wa kuweka kando matarajio yake binafsi.
Vyama vya upinzani nchini Kenya vimekubaliana kuungana na kusimamisha mgombea mmoja wa urais katika uchaguzi mkuu wa Agosti 2027, kwa lengo la kumzuia Rais William Ruto kupata muhula wa pili.
Uamuzi huo umefikiwa baada ya viongozi wakuu wa upinzani kufanya mazungumzo ya siku kadhaa katika eneo la Nairobi na Kiambu. Wameahidi kudumisha umoja wao katika mchakato mzima wa kumchagua mgombea atakayemkabili Ruto.
Katika taarifa yao ya pamoja, viongozi hao wamesema watatia saini Ahadi Binafsi ya Umoja pamoja na Mkataba wa Umoja wa Muungano. Makubaliano hayo yanatarajiwa kuwafunga viongozi wote kumuunga mkono mgombea atakayechaguliwa kupitia mchakato wanaoueleza kuwa wa haki, kuaminika na kukubaliwa na wote.
Kila kiongozi ameahidi kushiriki katika mchakato wa uteuzi na, baada ya mgombea kupatikana, kumuunga mkono kikamilifu na kumpigia debe katika uchaguzi wa mwaka 2027. Pia wameahidi kutohujumu mgombea huyo, kufadhili mgombea mwingine au kuchukua hatua zinazoweza kuugawa muungano.
“Tutaweka matakwa ya wananchi mbele na nyuma, na kisha tutawaletea mgombea mmoja,” amesema kiongozi wa upinzani Martha Karua.
