Na John Walter-Manyara
Ni habari njema kwa wananchi wa Kata ya Dirma, Wilaya ya
Hanang’ mkoani Manyara, baada ya Mkurugenzi wa Shirika la Maendeleo la ECLAT
Development Foundation, Bw. Peter Toima, kutangaza rasmi kuanza kwa awamu ya
pili ya ujenzi wa Shule ya Msingi Merekwa.
Akizungumza wakati wa kutangaza hatua hiyo, Bw. Toima
amesema kuwa ujenzi wa awamu ya pili unatarajiwa kuanza mapema mwezi Februari,
huku shule hiyo ikipangwa kukabidhiwa rasmi kwa Serikali tarehe 24 Novemba,
2026 baada ya kukamilika kwa viwango vinavyotakiwa.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi huyo, ECLAT Development
Foundation inatarajia kutumia jumla ya shilingi 286,302,200 katika ujenzi wa
awamu ya kwanza na ya pili ya shule hiyo, fedha zitakazogharamia ujenzi wa
miundombinu muhimu ya elimu.
Shule ya Msingi Merekwa ikikamilika itakuwa na ofisi za
walimu, madarasa yenye madawati, samani mbalimbali, jiko pamoja na matundu ya
vyoo kwa walimu na wanafunzi, hatua itakayoboresha kwa kiasi kikubwa mazingira
ya kujifunzia na kufundishia.
Bw. Toima amesema kuwa falsafa ya shirika hilo ni “hawavumi lakini wapo”, akisisitiza kuwa ECLAT haifanyi kazi kwa ajili ya kujitangaza bali kwa dhati ya kuwahudumia wananchi na kuleta mabadiliko chanya katika jamii.
Ameongeza kuwa hadi sasa, ECLAT Development Foundation
imefanya kazi katika mikoa sita nchini, katika zaidi ya wilaya tisa, ambapo
tayari zimeshajengwa takribani shule 60 za msingi, sambamba na ujenzi wa shule
za sekondari katika maeneo mbalimbali.
“Kikubwa tunachoomba ni ushirikiano, umoja na kila mmoja
kutimiza wajibu wake, ili maendeleo tunayoyataka yafikie jamii kwa haraka na
ufanisi,” amesema Bw. Toima.
Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Hanang’, Mheshimiwa
Asia Halamga, amemshukuru kwa dhati Mkurugenzi wa ECLAT Development Foundation
kwa uamuzi wa kujenga shule hiyo mpya ya msingi Merekwa, akieleza kuwa ni mradi
wenye tija kubwa kwa jamii za pembezoni, hususan kwa watoto wa jamii za
wafugaji ambao wamekuwa wakikumbwa na changamoto ya upatikanaji wa elimu.
Mheshimiwa Halamga amesema kuwa mchango wa ECLAT ni wa
kupongezwa kwa kiwango kikubwa na unaonesha jinsi mashirika ya maendeleo
yanavyoweza kushirikiana na serikali katika kufanikisha malengo ya elimu kwa
wote.
Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Hanang, Bw.
George Bajuta, ameahidi ushirikiano wa karibu kati ya Halmashauri na Shirika la
ECLAT Development Foundation, ili kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati
na kwa ubora unaokusudiwa.
Ujenzi wa Shule ya Msingi Merekwa unaendelea kuwa ishara
ya matumaini mapya, ukithibitisha kuwa pale panapokuwepo na dhamira ya kweli,
elimu inaweza kuwafikia hata watoto walioko maeneo ya mbali zaidi.
.jpeg)




.jpeg)


0 Maoni