F Mkurugenzi Simanjiro akutana na wadau wa Utalii. | Muungwana BLOG

Mkurugenzi Simanjiro akutana na wadau wa Utalii.


Na John Walter-Simanjiro

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro, Ndugu Gracian Makota, amekutana na kufanya kikao kazi na wadau mbalimbali wa uwindaji wa kitalii katika maeneo tofauti ya wilaya hiyo, kwa lengo la kujadili na kutafuta suluhu ya changamoto ya uvamizi wa vitalu vya uwindaji.

Kikao kazi hicho kilifanyika tarehe 27 Januari 2026 katika Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri, na kiliwakutanisha wadau wa sekta ya utalii wakiwemo Maafisa Kilimo, Maliasili na Mapato kutoka ofisi ya Mkurugenzi, Kamanda wa Uhifadhi Kanda ya Kaskazini – Arusha, Mkuu wa Utalii Kanda ya Kaskazini – Arusha, Maafisa Uhifadhi Wanyamapori, pamoja na wamiliki wa vitalu vya uwindaji vya Ilaroi Ranching LTD, Multicable Company LTD, Tanzania Big Game Safaris, Trophy Belt na Plains Game Adventures.

Lengo kuu la kikao hicho lilikuwa ni kujadili namna bora ya kukabiliana na changamoto ya uvamizi wa vitalu vya uwindaji, hali ambayo imekuwa ikiathiri shughuli za uhifadhi na uwekezaji wa kitalii katika eneo hilo.

Baadhi ya wamiliki wa vitalu vya uwindaji wamesema changamoto kubwa inayowakabili ni uvamizi unaofanywa na wananchi, hususan wakulima, wanapoanza msimu wa kilimo.

Wamedai kuwa baadhi ya wananchi wamekuwa wakiingia hadi ndani ya maeneo ya vitalu na kuanzisha mashamba mapya, hali inayosababisha wanyama kukimbia maeneo hayo kutokana na hofu, jambo linaloathiri shughuli za uwindaji wa kitalii na uhifadhi wa wanyamapori.

Akizungumza katika kikao hicho, Mkurugenzi Mtendaji Ndg. Gracian Makota amesema kuwa miongoni mwa suluhu ya kudumu ya tatizo hilo ni kuimarisha ushirikishwaji wa wananchi wanaoishi maeneo jirani na vitalu vya uwindaji.

Amesisitiza umuhimu wa kuitisha mikutano na vikao vya kimkakati vitakavyowakutanisha wananchi hao ili kuwapatia elimu kuhusu faida na umuhimu wa uwekezaji wa vitalu vya uwindaji wa kitalii, ikiwemo ajira, mapato ya Halmashauri na maendeleo ya jamii kwa ujumla.

Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro imeeleza kuwa itaendelea kushirikiana na wadau wa uhifadhi na utalii kuhakikisha changamoto hizo zinapatiwa ufumbuzi wa kudumu kwa maslahi ya uhifadhi wa rasilimali za asili na maendeleo ya wananchi.


@manyara_rs
@wizarayamaliasilinautalii
@ortamisemi
@tawa_tanzania
@gmakota

 

Chapisha Maoni

0 Maoni