Wizara ya ujenzi, uchukuzi na mawasiliano imewaagiza mafundi simu nchini, kujisajili katika Ofisi za Mamlaka ya mawasiliano Tanzania (TCRA), ili kudhibiti uhalifu unaofanyika kwa njia ya mitandao.
Kilio kikubwa kwa Watanzania wengi hivi sasa ni kupokea ujumbe mfupi wa maneno kupitia simu za mkononi, kutoka kwa baadhi ya matapeli wakiomba kutumiwa fedha kama njia ya kujikumu kimaisha.
Kutokana na wimbi hilo Naibu Waziri wa ujenzi, uchukuzi na mawasiliano Atashasta Nditie, amekutana na Chama cha mafundi simu mkoa wa Mwanza, ili kutafuta mwarobaini wa kutatua tatizo hilo, linaloendelea kuota mizizi kila uchao kutokana na mbinu za matapeli.
Katika mjadala huo mkurugenzi wa mawasiliano wa Wizara hiyo Mhandisi Clarence Ichwekelaza, na mkuu wa Mamlaka ya mawasiliano Kanda ya Ziwa (TCRA) Francis Mihayo, wakatumia fursa hiyo kuwaonya mafundi simu kutofanya kazi hiyo bila kusajiliwa.
Hatua ya onyo hilo imefuata baada ya kuthibitika kuwa wapo baadhi ya mafundi simu wasiokuwa waaminifu, ambao hubadilisha namba tambulishi za simu yani (IMEI) zilizotumika katika uhalifu.
Kwa muktadha huu kile kilio cha watanzania wengi cha kupokea ujumbe mfupi wa maneno kwa njia ya simu usemao, itafadhali ile pesa tuma kwa namba hii kugushi majina ya watu kwa lengo la kujipatia fedha kitapungua kama si kutoweka.
