https://monetag.com/?ref_id=TTIb Mgombea ubunge autolea macho ujenzi wa mtambo wa kuchakata gesi. | Muungwana BLOG

Mgombea ubunge autolea macho ujenzi wa mtambo wa kuchakata gesi.


 

Na Ahmad Mmow, Lindi.

Mgombea ubunge jimbo la Lindi kupitia chama cha Alliance for Change and Transparency (ACT-Wazalendo), Isihaka Mchinjita amesema akichaguliwa na kuwa mbunge wa jimbo hilo atapambana kuhakikisha ujenzi wa mtambo wa kuchakata gesi asilia ( LNG) unafanyika na kukamilika ili wananchi wanufaike na fursa zitakazo tokana na mtambo huo.

Mchinjita alitoa ahadi hiyo jana kwenye mkutano wa kampeni uliofanyika katika kata ya Makonde, halmashauri ya manispaa ya Lindi.


Alisema ujenzi wa mtambo huo unasuasua na haamini kama utakamilika bila kupatikana mwakilishi makini na mwenye uwezo wakuisukuma serikali unaotokana na uelewa wa mambo. Kwahiyo kunahaja ya kumchagua mtu atakayekuwa na uwezo ili ijenge na ikamilishe mradi huo wananchi wa jimbo hilo watumie fursa zitakazotokanana ujenzi huo.

Alisema kukamilika kwa ujenzi wa mtambo huo kutasababisha watu takribani 5,000 waajiriwe. Idadi ambayo nikubwa ikilinganishwa na idadi watumishi wa umma waliopo katika jimbo hilo la Lindi na hata mkoa wote wa Lindi ambao hawazidi 3000. Kwahiyo wafanyakazi wataofanyakazi kwenye mtambo huo watazalisha ajira nyingine kwa wananchi  wa jimbo hilo.

Alibainisha kwamba wafanyakazi 5,000 watakaofanya kazi kwenye mtambo huo mkubwa ambao uwekezaji wake utumia fedha nyingi iwapo kila mmoja ataamua kutumia shilingi 5,000 kwa ajili ya kununua chakula kwa mama lishe watakuwa

 wamewaingizia mamalishe hao takribani shilingi 25,000,000 kwa siku. Kiasi ambacho nikikubwa ambacho mamalishe hao watanunua bidhaa mbalimbali kutoka kwa wananchi wengine.

" Wachuuzi wa maji wote wataweza kuingiza takribani shilingi milioni tano kwa siku. Wauza mkaa wataingiza shilingi 35,000,000 kwa wiki. Kwahiyo mzunguko wa fedha utakuwa mkubwa. Nahilo linawezekana kwani kampuni ya Karafi ilibadilisha maisha ya watu wa Lindi kwa muda mfupi wakati inajenga barabara ya Mingoyo- Lindi," alisema Mchinjita.

Alisema kuna kila sababu ya mradi huo kujengwa na kukamilika haraka. Hasa ikizingatiwa kwamba mji wa Lindi hauna kiwanda kikubwa walau kimoja kinachoweza kutoa ajira za kutosha. Huku bandari nayo ikiwa imekufa na haieleweki ni mwaka gani itafufuliwa na watu waliouwa bandari hiyo.

Alisema japokuwa ujenzi wa mtambo huo unatija kwa wananchi wa jimbo hilo na taifa kwa jumla. Lakini wabunge waliotangulia inaonesha hawakujua umuhimu wa mtambo huo kwa wananchi waliokuwa wanawawakilisha. Hali iliyosababisha washindwe kuisukuma serikali ianze kujenga na kukamilisha haraka.

Alisema mji wa Lindi unahistoria ya harakati za kiuchumi na maendeleo kuliko mikoa mingine iliyokuwa inaunda kanda ya Kusini kabla ya Uhuru wa Tanganyika. Hali iliyosababisha wazee waliokuwa wanaishi katika mji huo waweze kujenga hata nyumba za ghorofa ambazo sasa watoto wao waliorithi wanashindwa kukarabati na kuzitafutia hati kutokana na ugumu wa maisha walionao. Huku mji huo ukigeuka kuwa kielelezo cha umasikini wa waTanzania.

Alisema jimbo hilo linachangamoto nyingi ambazo utatuzi wake unategemea uwezo, uelewa na ujasiri wa mwakilishi wa jimbo hilo ambaye atakuwa na uwezo wakuisukuma serikali bila kuogopa.

Mbali na hilo, mgombea huyo alitoa wito kwa wananchi wa jimbo hilo wenye haki na uwezo wa kupiga kura wakinyime kura Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwamadai kwamba wakichagua chama hicho watakuwa wamechagua kuishi kwa hofu kwa miaka mingine mitano ijayo.

Alisema katika kipindi cha utawala wa awamu ya tano wananchi wote wakiwemo watumishi wa serikali wameishi kwa hofu.Kwahiyo iwapo watakichagua tena chama hicho wajue wamechagua kuishi kwa hofu na mashaka badala ya furaha na utulivu kwa miaka mingine mitano.

" Pamoja na matukio mengi ambayo hayakupata kutokea katika awamu nyingine za utawala. Lakini hata watumishi wa serikali wanaishi kwa hofu ya kufukuzwa kazi muda wotewote. Wafanyakazi wanafukuzwa hadharani kwenye mikutano bila kufanyika uchunguzi. Hali ambayo inasababisha wafanyekazi bila kujiamini. Matokeo yake wanaharibu kutokana na hofu kubwa waliyonayo," alisema Mchinjita.

Kwakuzingatia hayo, mgombea huyo alidai kwamba wananchi  ni zamu yao kukitumbua CCM kama serikali ilivyowatumbua wafanyakazi na kuwatia hofu wananchi.

Post a Comment

0 Comments