DRC yawafukuza Wanyarwanda waliotoroka chanjo ya Covid-19

 


Takriban Wanyarwanda 100 ambao walikimbilia kisiwa kilichopo Ziwa Kivu katika nchi jirani ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ili kuepuka kupata chanjo za Covid wamerudishwa nchini kwao


Hata hvyo watu wawili wanadaiwa kutoonekana katika kundi hilo la Wanyarwanda 101 huku operesheni ya kuwasaka inaendelea.


Afisa wa Kisiwa cha Idjwi, Roger Ntambuka, aliiambia BBC kwamba mamlaka iliweza kufanya mazungumzo na Wanyarwanda hao ili kuwarejea nyumbani kwao.


"Hakukuwa na sababu ya Wanyarwanda hawa kubaki hapa. Tuliweza kuwashawishi," alisema.


Alisema raia hao wa Rwanda , ambao ni wanawake, wanaume na watoto, waliondoka kuelekea nyumbani kwa boti.


Gavana wa jimbo la magharibi mwa Rwanda alisema hakuwa na habari kuhusu Wanyarwanda waliokimbia na haijabainika kama mamlaka ilihusika katika kuwarejesha nchini kwao.


Wiki iliyopita mamlaka ya Burundi iliwafukuza zaidi ya Wanyarwanda 10 waliokuwa wameingia nchini humo kukwepa chanjo ya lazima ya corona na kuwarudisha nyumbani.


Raia wa Rwanda lazima wapewe chanjo ili kuruhusiwa kutumia usafiri wa umma, kwenda kwenye maeneo ya starehe(bar) na migahawa au kuhudhuria hafla za umma.

Post a Comment

0 Comments